Tuesday, March 30, 2010

KUDORORA KWA UFUMBUZI WA MGOGORO WA ZIMBABWE NA HADITH YA MWNAMKE MZINZI KATIKA BIBLIA
Katika Injili ya Yohane 8:1-11 kwenye maandiko matakatifu ya biblia tunapata kisa cha mwanamke mmoja mzinzi aliyepelekwa kwa yesu na mafarisayo na walimu wa sheria kwa lengo la kumjaribu yesu juu ya dhambi ya uzinzi aliyofanya mwanamke yule kwani kwa mujibu wa sheria zao mose aliwaamuru mwanamke kama huyo apigwe mawe hadi kufa. Walipozidi kummuuliza,yesu aliwajibu napenda kunukuu “Mtu asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza kumpiga jiwe”.Kisha akainama tena akawa anaandika ardhini.Wale mafarisayo waliposikia hivyo wakaanza kutoweka mmoja mmoja na kumuacha yesu peke yake na akiwa amesimama palepale.

Kila nikifikiria mgogoro wa Zimbabwe narejea kauli ya Yesu kristo aliyowapa wale wakuu wa sheria na mafarisayo wakiwa katika harakati za kutekeleza dhamira yao ya kumsulubu yule mwanamke mzinzi.Katika makala hii nashindwa kutafuta namna nyingine ya kuwafananisha viongozi wa kiafrika na wale mafarisayo na walimu wa sheria katika jitihada zao teketeke za kuutafutia ufumbuzi wa kudumu mgogoro wa Zimbabwe huku nyumba zao zikiwa chafu kwa kiwango kilekile na wakati mwingine kuuzidi huo wa menzao Mugabe.

Hakuna asiyetambua changamoto mbalimbali zinazoikabili nchi hii iliyo kusini mwa afrika ya jangwa la hasara.Mgogoro wa Zimbabwe kila kukicha unazidi kuchukua sura mpya na madhara ya kibinadamu yanazidi kuwa makubwa. Ukijaribu kuangalia jitihada zinazofanywa na wakuu wa nchi za kiafrika hazilangani na wala kutoa matumaini ya kupatikana suluhu ya haraka katika mgogoro huo ambao unaendelea kugharamu maisha ya wazimbabwe walio wengi na wasio na hatia.

Viongozi wa kiafrika wanatambua kwa undani udhaifu wa mwenzao raisi Mugabe lakini nani mwenye ujasiri wa kukemea ubabaishaji katika serikali yake wakati wenyewe huendekeza ustaarabu wa kizandiki katika dola wanazoziongoza na kuendelea kila siku kusuka mikakati ya kuangamiza demokrasia change ambayo ilianza kupenyeza katika karne ya ishirini ambayo kimsingi ni changamoto mahsusi katika kuchochea maendeleo ya nchi hizi ambazo zinazidi kulowea katika lindi la umaskini mkubwa.

Vyombo vya kikanda katika bara la kiafrika vinabaki kuwa sehemu ya wakubwa kukutana na kuonyeshana ufahari wa kirasilimali wa nchi husika na ukwasi wa watawala huku wakisahau na kuweka kando agenda muhimu za kuwaletea wananchi wake maendeleo na kuimarisha amani.Katika jumuiya ya maendeleo ya kusini mwa Afrika na umoja wa Afrika kuna vyombo mahsusi kwa ajili ya kushughulikia matatizo kama haya ya Zimbabwe.

Vyombo hivi vimebaki kuwa vya kuhifadhiana udhaafu wa wenzao huu wananchi wao wakiendelea kuteseka kila kukicha na kuziacha nchi moja moja kukemea ubabaishaji huo ambazo kimsingi zinakosa nguvu za kukemea uzandiki wa kimadaraka unaowakabili viongozi au wakuu wan chi za kiafrika na hivyo kutoa uhalali wa kuwepo kwao.

Botswana imekua ni nchi pekee kukemea udhaifu huu wa serikali ya Zimbabwe chini ya ubabaishaji dhahiri wa rais Mugabe bila kificho au kuoesha unafiki katika kutafuta ufumbuzi wa mgogoro huo lakini jitihada hizo zilifunikwa na kikao cha wakuu wan chi za kiafrika kilichofanyika misri mwaka jana siku chache baada ya uchaguzi wa marudio wenye utata ambao umoja wa Afrika ulishindwa kuonyesha dhamira ya dhati katika kukemea ubakaji wa demokrasia ulionyeshwa na rais Mugabe.

Nchi za kiafrika zimekuwa vinara wa kubuni mikakati isiyotekelezeka ili kuwashwashi mabwana wakubwa wa nchi za magharibu kuendelea kuzisaidia.Hakuna asiyeamini mkakati uliobuniwa na waafrika wenyewe wakiongozi na wanadiplomasia mahiria kama Thabo Mbeki,Abdulay wade,Olesegun obasanjo wa kufanyia tathmini utekelezezaki wa utawala bora katika dola za kiafrika,maarufu kama APRM ungeshindwa kuwa ni msingi imara wa kuichukulia hatua Zimbabwe ambayo imedhihirika kuzikiuka katika viwango vya kutisha.

Katika hali ya kushangaza rais Mugabe anatoa kauli ya kukanusha kuwa nchi yake haina tatizo la kipindupindu wakati vyombo vya habari vya ndani ya nchi,afrika na dunia vinaripoti ongezeko la tatizo hilo kila kukicha na watu wakendelea kupoteza maisha bila hatia yoyote huku vioongozi wa kiafrika wakiendelea kujigamba mbele ya mataifa ya nje kuwa jukumu la kutatua mgogoro huo liko mkononi mwa waafrika wenyewe wakati kimsingi wamekosa sifa za usafi katika kushughulikia tatizo ambao wao kimsingi wamekua wakiyaendekeza katika nchi zao.

Kueendelea kuvilaumu vyombo vya habari vya kimataifa kuwa vinachochoe au kutia chumvi hali halisi ya matatizo nchini Zimbabwe ni kutaka kukwepesha ukweli ambao kila mtu anaona.Rais Mugabe amekua akitumia hili kama njia ya kujisafisha kwa wananchi wake na kwa viongozi wenzake wa kiafrika ambao kimsingi wameshamchoka ila inabaki dhana ya kutunziana heshima.

Mbinu chafu alizotumia Mugabe katika kujitwalia madaraka na ambazo ameendelea kuzitumia kuiongoza dola ya wanazimbabwa ni mfano tu na kiwakilishi cha uzandiki na ubabaishaji katika nchi mbalimbali za kiafrika hivyo kumfanya apate kiburi cha kukataa shinikizo kutoka kwa nchi nyingine za kiafrika kuingilia mgogoro wake.

Raisi Mugabe ni kama anawauliza viongozi wenzake,ni nani msafi anitupie mawe?Nani ambaye hatendi dhambi anyanyue jiwe anirushie?Nani asiyeiba kura asimame aniambie?Nani asiyekiuka haki za binadamu katika nchi yake?hakika ni mambo mengi yanayofanywa na vioongozi wa nchi za kiafrika ambazo yanarandana na haya yanayotokea Zimbabwe kwasasa nap engine hata kuzidi yanayotokea Zimbabwe.

Pembe zote za afrika iwe kaskazini,kusini,mashariki na magharibi watawala wa nchi zetu wamekuwa wakendesha ubabaishaji kama huu anaoufanya raisi mugabbe na kimsingi hakuna msafi wa kusimama mbele ya hadhara ya kukemea hali hiyo na kuchukua hatua dhidi ya mtawala huyu ambaye anazidi kutia doa ustawi wa demokrasia yetu change ambayo imeanza kuchanua miaka ya tisini.

Umoja wa afrika ulio chini ya rais wa Tanzania mheshiiwa Jakaya Mrisho kiwete iliongoza opereshni ya mafanikio katika kumuondoa madarakani kanali Mohamedi Bakari wa visiwa vya anjuani komoro kwa mafanikio makubwa lakini hatma ya mgogoro wa Zimbabwe hadi sasa haijulikana licha ya kuwa madhara anayosababisha \mugabe kwa kwa wananchi wake ni makubwa zaisdi ya yale aliyokuwa anasabibisha Bakar huko anjuani.

Sina maana kuwa nguvvu za kijeshi ni muafaka katika utatuzi wa mgogoro huoo wa Zimbabwe ila dhamira na utayari wa kutautua mgogoro huo mbona haupo.Nani asiyejua kuwa chanzo cha mgogoro huo ni raisi Mugabe mwenyewe?Nani asiyetambua wananchi wanateseka kwa mambo ambayo kimsingi hawakupaswa kuyakabili?

Viongozi wetu wamekuwa wakijitapa kila kukicha kuwa matataizio ya kiafrika yanapaswa kutatuliwa na waaafrika wenyewe lakini cha kustaajabisha hadi sasa hakuna anayeonyesha nia na uwezo wa kuthibtisha umakini wa kauli hizo kimatendo.Hakuana sababu ya kutafuta umaarufu katika maneno ambayo hayajidhihiriushi katika matendo yenye muelekeo wa kutatua matatizo ya nchi zao.

PROFESSOR HAROUB OTHMAN DEMISE: A HUGE INTLECTUALL LOSS

It was Sunday 29th June 2009 at around 3.00 pm when messages from colleagues at the institute of development studies of University of Dar es salaam started flocking into my phone all reading ‘professor Haroub Othman is no longer with us’, ‘a great intellectual loss’, ‘our academic father has gone’ all of which trying to express the sorrowful loss of such a great guru not only in laws but also politics, diplomacy, economics, democracy, human rights and social welfares.

While the government is struggling to widen access of more people to earn university education, the country is experiencing another huge loss of its prominent intellectual resource that was expected to push forward the mission. In a three years time, following the death of comrade professor Chachage whose gap remains unfilled, the academic community is again thorned in almost the similar way because these are people we wish they could live longer for the current and future generation to benefit not only from their intellectual but also charismatic wisdom.

There is no doubt that, the news were shocking to everyone who once had an opportunity to meet him, talk to him and/or even listen him through the media where he diligently and heartedly spent most of time dishing out important messages to his fellow citizens. He had a passion for his country and had a vision of what Tanzania should be in terms of development; respect the rule of law, good governance and social welfare at large.

I started hearing this great name while I was in standard seven in the year 1993 when schooling at mbokomu primary school in Moshi rural district but my attention was peculiarly drawn two years later in 1995 when he was heading the United Nations team to facilitate the formation of the transitional government (setting up governance structure) in Liberia after many years of wars and unrest.

My thought by that time was sharpened and my appetite to advance and excel in the career ladder was wet by the late professor Othman knowing that the great responsibility bestowed on him by that time was not just only the kind of individual respect he was earning but also the professional legacy that his institution and country will live up with for hundreds of years ahead.

He was a role model for the majority of us in the academic community and almost every student wanted to register a course that the late comrade Othman was facilitating. I personally felt blessed when he taught me a course on governance and development during my undergraduate studies in the years 2002/2003 and when I returned for my master’s degree in development studies in the year 2008 where he taught me socialist political ideas in development.

The late professor Othman was an inspirational to the majority of us today. Not only to those who has gone to school or taught by him but to anyone whose desire and optimism for a better and just society stands beside him. He always wanted to see things going righteously in our dear country and everyone gets the desirable share of our national cake.

His spirit was molded by the fear of God, his professional and/or intellectual mighty was sharpened and blessed by the wishes of those vulnerable groups in the society whose existence rest upon the voice of people like professor Othman who firmly stood and emphasized the need to anchor our political freedom in addressing those obstacles that impedes human development such as inequality, corruption, poor governance, social and political exclusion that will enable all the people to have voice in what happens in their communities regarding their well being.

Professor Othman was not only an academician and/or activist but also the father at the hill. I called him a father for one reason, he was always ready at any times to meet and talk to his family (university students). He was reachable and welcoming at all times and places be it in the corridors, his offices, on the road, his cell phone and at any point you happen to meet him.

A lot can be said and written about professor Othman but the most important is to make sure his legacy live with us especially in setting a collective vision of governing our dear nation which he always felt proud to be part of it. His interests in dialogue as well as strong belief in socio-economic and political justice should reaffirm our responsibility as a nation to stand for issues that will bold our unity and ensure the thriving of peace.

Rest in peace comrade, rest in peace our father, and rest in peace our role model.
NGUVU YA MALUMBANO YA SERIKALI NA MENGI IELEKEZWE KWENYE VITA DHIDI YA MAUAJI YA ALBINO

Jukumu moja kubwa kwa serikali yoyote ile duniani ni kusimamia uhai wa watu wake na mali zao.Haiingia akilini kuona serikali makini ikitelekeza wajibu wake huu mkubwa na kuanza kujihusisha katika malumbano yasiyo na tija kwa wananchi wake na kuwaacha makumi kwa mamia ya raia wake wakipoteza uhai ambao ni haki yao ya msingi na ambao serikali iliapa kuulinda na kuutetea.

Nadiriki kuamini kuwa kauli ya serikali iliyotolewa na waziri wa mambo ya ndani ya nchi mheshimiwa Lawrence masha dhidi ya mwenyekiti mtendaji wa makampuni ya IPP mzee Reginald mengi ya kumpa siku saba athibitishe madai yake aliyotoa kuhusu waziri mmoja kijana anyesuka njama za kumhujumu katika shughuli zake za kibishara ni ushahidi mwinginbe ulio wazi kuwa serikali yetu imekosa agenda muhimu za kusimamia.

Sitaki kuamini madai yaliyotolewa na mzee mengi yanageuka kua agenda muhimu kwa serikali makini. Serikali isiyo na agenda mara nyingi kama si zote imekua ikitapatapa kwa kila jambo linaloibuka hata wakati mwingine likiwa halina maana wala tija katika ustawi wa kijamii au kiuchumi wa jamii husika.Sitaki kuaamini kuwa madai ya mengi yaliyoibiliwa hivi karibuni yanapaswa kupewa nguvu kubwa kama inavyoelekea kupewa hivi sasa na wadau wa serikali na vyama vya siasa ambao mwisho wake ni kuendelea kuwagawa wananchi na kuwayumbisha na hatimaye kutumbukia katika mijadala isiyo na maana wala heri kwa taifa letu.

Waziri Masha ni mdau mkuu na muhimu na aliyepewa dhamana katika kusimamia usalama wa raia na mali zao na anapaswa kubuni mikakati na miongozo katika vita dhidi ya ukatili unaoendela kwa watanzania wenzetu wenye ulemavu wa ngozi wanaojulikana kwa sasa kama Maalbino na siyo kujitumbukiza katika malumbano yanayoelekea kuchafua roho zetu na kusahaju jukumu muhimu alilopewa la kusimamia uhai na usalama wa raia walio wengi haswa maalbino walio katika hatari ya kuotokomea

Jamii hii ya watanzania hawa walemavu wa ngozi wamepoteza matumaini ya kuishi na hawana uhakika kama wataiona kesho kwani maisha yao siku zote yako hatarini.Nguvu zao za kujilinda dhidi ya ukatili huu ni dhaifu ukilinganisha na za maadui wao ambao imekuja kubainika kuwa baadhi yao ni askari ambao kimsingi walipaswa kuwalinda.

Serikali inatoa siku saba kwa mtu mmoja kuthibitisha madai ambayo mwisho wake utaishia kule kule kwa malimbano ya awali kati mwenyekiti huyo na mbunge wa mkuranga mheshimiwa Adam malima na huku maalbino wakiendelea kupoteza maisha bila mtetezi wa kweli na haki yao ya msingi ya uhai ikiendelea kuchezewa danadana.

Waganga wa jadi wanaendelea kutamalaki na kuchochea mauaji ya watanzania wenzetu wasio na hatia huku serikali ikijihusisha katika malumbano yasiyo na msingi na kusahau agenda zake za kutetea maisha ya wananchi wake na kuandaa mazingira salama ya wao kujishughulisha na kujiletea maendeleo yao wenyewe.

Serikali inaanza kupoteza muelekeo na kubaki na agenda moja kila kukicha ya kujisafisha dhidi ya kashfa na madhambi yanayowaandama watendaji wake mmoja mmoja au serikali nzima kwa ujumla.Nani kasema mengi ni muhimu kuliko maisha ya albino wanaopteza maisha kila kukicha?Nani kasema waziri mtuhumiwa ni muhimu kuliko maisha ya ndugu zetu hawa wanaoangamia bila sababu?Nani kasema usafi wa serikali machoni mwa watanzania ni muhimu kuliko uhai wa wananchi wake?

Vyombo vya habari navyo vinaelekea kupotezwa muelekeo na kujikuta vinajinasa katika mtego wa malumbano na kupoteza dhima nzima ya habari na umuhimu wake katika kupinga vita maovu kama haya dhidi ya watanzania wenzetu wenye ulemavu wa ngozi.Maisha ya maalbino yanafanywa kama ni mambo yasiyo na msingi na kuendekeza malumbano ya kisiasa ambayo ni wazi kuwa hayana tija katika maisha ya watanzania na katika uhai wa ndugu zetu hawa.

Juzi mlemavu mwingine wa ngozi wa kijiji cha Nkindwabye willayani Bariadi ameuawa kikatili kwa wauaji kutoweka na kichwa na miguu yake yote miwili.Hakika maisha ya ndugu zetu hawa yanaonekana hayana thamani na nguvu inayoelekezwa kuyalinda nachelea kusema kuwa inatosha na yenye nia thabiti ya kuyatokemeza kabisa.

Siku saba alizopewa mzee mengi kama nilivyodokeza hapo juu zingepaswa kuelekezwa katika kuokoa maisha ya ndugu zetu hawa ambao kimsingi wamebakia bila mtetezi wa kuaminika na mwenye nia ya kuwafanya waishi maisha ya amani na utilivu wa moyo kwa wakati wote ule kwani serikali inasahau jukumu lake na vyombo vya habari navyo halikadhalika.

Serikali siku zote imekua ikiaminika kuwa na mkono mrefu ambao una nguvu ya kuwafuata wale wote wanaojihusisha na uovu na kuwaleta katika vyombo vya sheria.Kutumia nguvu hiyo kwa mtu mmoja kwa lengo la kujisafisha machoni mwa mwananchi huku makumi ya raia wengine walemavu wakiendelea kupoteza maisha yao ni aina nyingine ya ubabaishaji.

Wizara ya mambo ya ndani ambayo waziri masha anaisimamia inapaswa kuwa mstari wa mbele katika kupiga vita unyama huu ambao unaendelea kulitia doa taifa letu ambalo siku zote tumekua tukijisifia kuwa kinara wa amani na utulivu.Si busara kwa seriakli kuendelea kutumia nguvu kubwa kwa mtu mmoja na huku tukiacha mamia ya wananchi wetu wakiangamia.

Malumbano haya hayana muelekeo mwema kwaiyo ni vyema wadau wote washirikiane na waelekeze nguvu zao katika kuokoa maisha ya watanzania wenzetu.Nguvu kubwa ya kutumia vyombo vya habari katika kuchafuana na kujisafisha ni busara ikaelekezwa katika vita ya kupinga mauaji ya maalbino.
gasper_materu@yahoo.ca
RAISI KIKWETE USIWAVUMILIE VIONGOZI WASIOWAJIBIKA

Rais kikwete wakati anahutubia bunge la Jamuhuri ya muungano wa Tanzania manamo tarehe 30 december 2005 mara baada ya kuibuka mshindi wa nafasi ya urais katika uchaguzi wa tatu chini ya mfumo wa demokrasia ya vyama vingi alitoa hotuba ya kusisimua na kuhuisha matumaini ya watanzania ambao wengi wao tayari walikuwa wamekata tamaa juu ya mustakabali wa maisha yao katika nchi yao ambayo wengi wao wamejitoa kwa dhati ya moyo wao wote kuijenga.

Mambo makuu mawili ambayo mheshimiwa rais alitumia mda mwingi kuyafafanua na kuyasisitiza wakati wa hotuba yake ile ni kwanza kuilinda na kudumisha amani na usalama wa nchi ambavyo waasisi wa taifa hili walitumia mda na nguvu nyingi kuvipigania na jambo la pili lilikua kuboresha maisha ya watanzania ambao walionyesha imani kubwa kwake kwa kumchagua kwa kura nyingi kitu ambacho hata raisi Kikwete mwenyewe alikiri kuwa ni deni kwake.

Binafsi namuheshimu sana rais kikwete na kutambua dhamira yake kama raisi katika kuwaletea wananchi wake maendeleo. Napenda kusema pia nakiheshimu chama cha mapinduzi kwa kuzingatia historia yake na waasisi wake katika jitihada za kuliongoza taifa katika wakati mgumu na kuwatumikia wananchi wake ambao waliendelea kuonyesha imani kwacho kwa miongo kadhaa sasa. Nimeamua kulisema hilo mapema ili ili watu wasiendelee kujenga hoja mufilisi pale tunapoandika mambo ambayo wenye njaa ya fikra thabiti wamekuwa wakiendelea kutunyooshea vidole kuwa tuna chuki na watawala na chama tawala ambacho kimsingi kimetukuza hata sisi.

Rais Kikwete wakati wa hotuba yake ile aliliambia bunge kuwa ‘Urais wake hauna ubia na mtu’. Maneno yale ni kama alikuwa anawaambia wasaidizi wake kuwa hatawavumilia pindi watakapoonekana kwenda kinyume na misingi ya kiutumishi unaolenga kuwaletea a wananchi maendeleo, kuwaondolea kero zao na hatimaye kujenga taifa imara lenye mikakati thabiti ya kujiondolea umaskini na kulinda misingi ya haki za watu na utawala wa sheria.

Ni kweli iliyo wazi kuwa raisi kikwete binafsi hawezi kulivusha taifa hili katika bahari iliyojaa changamoto mbalimbali kama umaskini, rushwa,maradhi, ujinga, unyimwaji haki na kuporomoka kwa maadili ya jamii ambayo imepelekea kuibuka kwa vitendo vyenye kuashiria uvunjifu wa amani na utulivu wan chi yetu ambayo kwa kipindi kirefu imefanikiwa kijijengea heshima katika jumuia za kimataifa.

Kwa kuzingatia ukweli huo ni budi kwa raisi kuteua watu ambao anawaamini kuwa na uwezo wa kumsaidia katika kutekeleza majukumu aliyopewa na wananchi ambao kimsingi ndiyo waajiri wake wakuu na mwisho wa siku atawajibika kwao. Changamoto ya kuwapata watu hao ni kubwa lakini kwa kushirikisha vyombo vyake vya usalama tulitegemea kuwa inaweza kuwa rahisi na kuwapatia wananchi watu ambao wanaongozwa kwanza na maadili ya utumishi uliotukuka ambao umejikita katika misingi ya maadili ya utoaji huduma.

Ukiwa mfuatiliaji wa mambo yanavyokwenda katika nchi yetu lazima utawaonea sana huruma viongozi wakuu wa nchi kama raisi, waziri mkuu au makamu wa raisi wanavyohangaika huku na kule katika kutatua kero ambazo kimsingi wasaidizi wao kama mawaziri,wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya wangepaswa kuzisimamia kwa nafasi zao na kuhakisha wananchi wananishi maisha ya raha mustarehe kwani rasilimali za kufanikisha hayo wanazo.

Ukiangalia mambo yanavyokwenda unaanza kupatwa ujasiri wa kuhoji kauli ambazo viongozi wetu wakuu kama raisi ambzo wamekuwa wakizitoa. Ahadi aliyoitoa rais kikwete ya kutowavumilia viongozi au watendaji wababashaji inapaswa kujidhihiri kwasasa ambapo kero za wananchi zimekuwa nyingi bila kuwepo matumaini yoyote ya kutatuliwa hukutukiendelea kushuhudia mbwebwe za wasadizi wake kama mawaziri ambazo kimsingi hazilengi kuwaondolea wananchi matatizo yao.

Huwa napenda kuikariri mara kwa mara kauli ya raisi kikwete aliyiotoa bungeni kwa lugha ya kiingereza nadhani alitka kuonyesha msisitizo na ningependa kuinukuu ‘I might be wearing a smile but I am firm on issues’. Hiyo ni kauli ya raisi kikwete ambayo nadhani ililenga kuwataadharisha wasaidizi wake ili kuonkama ile ya kuwatisha watendaji wake kuwa hatawavumilia pindi watakapoonekana hawatimizi wajibu wao wa kuwatumikia wananchi na kuwaondolea kero zao na hatimaye kufanikisha kauli mbiu ya maisha bora kwa kila mtanzania na sio wana CCM pekee.

Tathmini katika utendaji wa wasaidzi wa raisi kikwete inaacha maswali mengi kuliko majibu. Iko wapi meno ya raisi kikwete? Wasaidizi wake wamekubwa na nini? Wananchi wategemee nini katika kipindi hiki kifupi kilichobaki cha uongozi wake? Je,matatizo au kero za wananchi wetu ni laana isiyoweza kufutika? Tunahitaji nini kuwafanya wasaizi wa viongozi wetu wakuu watimize wajuibu wao?

Ni kwanini rais kikwete uwape fursa wanasiasa,wapinzani wako na wale wasio na mapenzi ya kweli na wewe kuendelea kuhoji uwezo wako ambao kimsingi naamini ni mkubwa kwa makosa ya watendaji au wasaidizi wako ambao kimsingi uwezo wa kuwashughulikia unao ambao una nguvu na baraka za kikatiba. Naamini utakua unaufahamu ule msemo wa wahenga unaohoji busara na ningependa kunukuu

“Busara ya mwenye nyumba kufuga mbwa kisha usiku wa manane anatoka kubweka
mwenyewe”

Ukiangalia muundo wa bajeti zetu unapatwa na ghadhabu kubwa hasa unapoamua kulinganisha fedha zilizotengwa kugharamia matumizi ya kawaida na shughuli za kimaendeleo katika nchi yetu. Sina nia ya kupinga mantiki ya mgawanyo huo ila nakerwa sana na kiasi kikubwa kilichotengwa kuwahudumia wasaidizi hao kama mawziri,wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya ambao wengi wao wamekuwa wakishindwa kutimiza wajibu wao katika maenneo yao ya kazi na hivyo kukwamisha juhudi za serikali kuwaletea wananchi maendeleo na kuwaondolea kero zao ambazo zimekuwa zikichangia kudumisha maisha yao kwa kipindi kirefu.

Mimi sioni mantiki ya viongozi wetu wakuu kama rais,waziri mkuu na makamu wa raisi kuendelea kukubali kusulubiwa kama yesu kristo kwa makosa ambayo kimsingi yanachangiwa na wasaidizi wao. Inasikitisha sana pale mtu unapoamua kukadidiso kwa wananchi ni mawaziri gani ambao wao wanadhani wanatekeleza majukumu yao kwa ufanisi unashindwa kupata majina zaid ya kumi(10) katika baraza lenye mawaziri zaidi ya hamsini (50).

Hali ni hiyo hiyo kwa wakuu wa mikoa na wilaya ambao kimsingi ndo wako karibu na wananchi. Kila siku vyombo vya habari vimekuwa vikiripoti madhila wanayokabiliana nayo wananchi kana kwamba hakuna watu waliopewa majukumu ya kuwasaidia hivyo kuwafanya wajione kama ni yatima katika nchi yao.Kero nyingi ambazo zimekuwa zikiendlea kuwasumbua wananchi kwa kiasi kikubwa zimechangiwa na kutowajibika kwa viongozi au wasaidizi hao ambao wengi wameota pembe na kiburi kitukufu kwani wanajua kuwa hakuna atakayewachukulia hatua.

Vitisho pekee vinavyotolewa na viongozi wakuu dhidi ya wasaidizi au watendaji wababaishaji havitoshi kwani waswahili walishasema sikio la kufa halisikii dawa kwahiyo wakati wa kuwachukulia hatua madhubuti na kali wale wote wanaondelea kuzikalia ofisi za umma na kuendelea kufuja rasilimali za umma bila ya kutimiza wajibu wao wa msingi wa utumishi kwa wananchi umefika na hatpuaswi kusubiri zaidi ya hapa kwani wananchi wanaendela kuteseka.

Hatua aliyochukua raisi kikwete ya kumfukuza mkuu wa mkoa wa mara kanali Enosi mafuru katika sherehe za kufungua hoteli mpya ya kitalii huko Serengeti ili arudi kuwaondelea kero za mapigano wananchi wake ni za kupongezwa lakini hazipaswi kuishia hapo. Wale watumishi ambao wanaonekana kushindwa kutekeleza majukuu yao hawapaswi kufumbiwa macho na kuendelea kulelewa huku wananchi wakiendelea kupoteza maisha na mali zao.

Kwanini fimbo uliyotumia kumchapia mkuu wa wilaya ya karagwe mheshimiwa mnali usiitumie kuwachapia watendaji wengine ambao kwa wakati huu imedhihirika kuwa wako wengi? Kwanini ukubali kujenga hali ya kutoaminika kwa wananchi wako waliokupa dhamana ya kuwatumikia? Kwanini watu waendelee kudhani uamuzi ulioufikia kumuachisha kazi mnali ulikuwa wa kisiasa na sio wa dhamira yako ya kiuongozi? Au unataka wapinzani wako waendelee kupata ya kusema kuwa ulimwachisha kwasababu sio mwanamtandao mwenzako?

Matokeo ya kuendelea kulea uvundo na ugoigoi wa watendaji ni mabaya sana ambayo kimsingi kwa mtu yoyote mwenye akili hapendi kuona yakitokea. Viongozi hawapaswi kusubiri hadi wananchi wakate tamaa na kuanza kujichukulia sheria mkononi au uamuzi wa kuanza kujiongoza wenyewe. Matukio yaliyoshuhudiwa mkoani mbeya katika kipindi cha wiki mbili cha mapambano ya polisi na raia yanapaswa kufungua macho ya watendaji kwani utamaduni wa wananchi kuvamia vituo vya polisi haujazoeleka nchini mwetu na ni ishara ya wananchi kupoteza imani kwa wale waliopewa dhamana za kuwaongoza.

Huku vyama vya upinzani vikjijaribu kuja na mikakati ya kuwahamasisha wananchi kwa kutumia opersheni mbalimbali kama vile operesheni sangara na operesheni sangara mimi namsihi rais kikwete aje na “Opersheni ng’oang’oa” itakayolenga kusafisha na kung’oa mizizi yote ya kutowajibika kwa viongozi wabovu ili kukinusuru chama tawala na kuliokoa taifa lisiangamie kwa mambo ambayo yako ndani ya uwezo wetu.

Huu si wakati wa ushabiki wa kisiasa katika mambo ambayo yanahusu maslahi ya kitaifa na ustawi wa jamii yetu ya kitanzania. Mifumo ya wazi tathmini ya upimaji utendaji kazi wa viongozi wetu na utoaji motisha (Performance based incentives) unapaswa kupewa mkazo ili kuhakikisha rasilimali wanazotumia viongozi wetu zinalingana na tija wanayoileta katika kuwaletea wananchi maendeleo ambao kimsingi ndiyo waajiri wao.

Mungu ibariki Tanzania yetu na viongozi wetu.
MCHAWI WA MAENDELEO YA AFRIKA NI WAAFRIKA WENYEWE

Bara la Afrika linaendelea kupita katika wakati mgumu kwa miongo kadhaaa sasa. Wananchi wake wanashindwa kujua ni lini ndoto zao za kuishi maisha bora baada ya kuteseka kwa kipindi kirefu zitakuwa kweli. Kila kukicha wananchi wanaendelea kukata tamaa na kubaki wakiitamani jana kuliko leo na kesho kwani mambo yanazidi kwenda mrama na hakuna dalili ya muujiza kutokea utakaowafanya wao wajihisi ni sehemu ya dunia ya sasa inayafaidi matunda ya sayansi na teknolojia katika karne hii ya ishirini na moja.

Kumekuwa na mijadala mbalilmabi inayoendelea katika kile kinachoonekana kumtafuta mchawi wa matatizo yanayoendelea kulitafuna bara letu hili kwa mda mrefu ambayo imeibua mitizamo tofauti. Kwa upande wa Afrika, historia imeendelea kutumiwa na viongozi wetu kama chanzo cha matatizo hususani ya umaskini yanayoendelea kulikabili bara letu na wananchi wake licha ya miongo kadhaa kupita tangu nchi hizi zijipatie uhuru wake kutoka kwa wakoloni.

Ni kweli kwamba ukoloni na biashara ya watumwa ulichangia kwa kiasi fulani kudumaza maendeleo ya bara letu la Afrika lakini hakuna mantiki ya kuendelea kuwa watumwa wa historia na kujifunga katika fikra ambazo kimsingi hazina mashiko kwasasa kwani ni kipindi kirefu kimepita kwa sisi kuweza kukaa na kujipangia dira ambazo tunaamini zingetupeleka kule tunapotaka kufika.

Wakati viongozi wetu wa bara hili wakiendelea kutafuta visingizio na kupiga ramli kumtafuta mchawi anayekwamisha ustawi wa maendeleo ya wananchi wao na nchi zao wanakumbushwa ukweli mmoja ambao wengi wao wamekuwa wakiendelea kuukwepa kuujadili kwa uwazi kwa kipindi kirefu sasa na kubakia kubwabwaja visingizio ambavyo kimsingi havilengi kuujua ukweli wa mambo bali kujijengea uhalali kwa wananchi wao kwamba matatizo ya nchi zao hayatokani na wao kutowajibika ipasavyo.

Akihutubia bunge la jamuhuri ya watu wa Ghana Julai 11 2009 wakati wa ziara yake ya pili katika bara la Afrika baada ya ile ya Cairo,rais Barrack Obama wa marekani ambaye ana asili ya Afrika aliamua kuwapsulia ukweli viongozi hao wa afrika ambao kwa kipindi kirefu sasa wamekuwa wakishindwa kuukabili ukweli huo kwa uwazi unaostahili. Raisi Obama aliliambia bunge la Ghana na napenda kutoa tafsiri isiyo rasmi “Kitu kinachokwamisha maendeleo ya Afrika ni tabia ya viongozi kuendelea kutoukubali ukweli kuwa utawala mbovu na rushwa ni sababu kuu katika hilo”

Ni ukweli ulio wazi kuwa dhana ya utawala bora imeendelea kupewa tafsiri finyu na kufananishwa kama utamaduni wa kimagharibu ambao hauna nafasi katika mazingira yetu ya kiafrika. Watawala wetu wameendelea kudhani kuwa,kwa kufanya changuzi katika nchi zao ni kielelezo mahsusi cha wao kutekeleza dhana hiyo kitu ambacho kwa kiasi kikubwa kimeendelea kuwapa ujasiri wa kujitangaza mbele za jumuiya za kimataifa kuwa wanatekelezo kwa vitendo dhana hiyo.

Ukijaribu kuoanisha hoja hizo na hali inavyokwenda hupati shida ya kutambua ni kwanini watawala wa bara hili wanapata shida ya kutambua dawa za matatizo yanayozikabili nchi zao kwa kipindi kirefu sasa na raisi kikwete anaweza kuwa mfano mahsusi katika hilo. Wakati alipohojiwa na chombo kimoja cha habari cha magharibi alisema hata yeye hajui kwanini bara letu la Afrika na hususani nchi yetu vimeendelea kulowea katika dimbwi la umaskini licha ya kuwa na kila rasilimali zinazohitajika katika kuwaletea wananchi wetu maendeleo kwa kasi.

Tunatambua kuwa njia pekee ya kuliondoa tatizo ni kukubali kulikabili tatizo lenyewe na siyo kujifanya kuwa wewe au mimi siyo sehemu ya tatizo lenyewe. Dhana ya utawala bora ni pana na haipaswi hata kidogo kurahisishwa na kuonekana kama inaishia katika uratibu wa chaguzi mbalimbali ambazo kimsingi pia zimekuwa hazifuati misingi ya kidemokraisa.Hii ni tafsiri finyu ambayo kama haitapata nafasi ya kujadiliwa kwa upana itaendelea kutoa uhalali kwa viongozi wasiofaa kuendelea kukalia viti bila uwezo wa kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Kama alivyogusia raisi Obama,bara letu na viongozi wake kwa miaka kadhaa sasa wamekuwa wakiyatupia kisogo mambo muhimu kama utawala wa sheria na unaoheshimu haki za binadamu, uadilifu na uwajibikaji wa viongozi, uwazi katika uongozi au uendeshaji wa serikali, ushirikishwaji mpana wa wadau katika kufanya maamuzi ambavyo kwa pamoja vinakamilsha dhana nzima ya utawala bora.

Ni ukweli ulio dhahiri kuwa misingi hiyo licha ya kuwa ni ajenda ya siku nyingi inayopiganiwa na mataifa yanayoendelea na wanaharakati wa kimaendleeo imekuwa ikiukwa kwa kiwango kikubwa katika nchi zetu za kiafrika na viongozi wetu ndo wamekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kuwa haipati nafasi ya kumea katika bara hili kwani inapinga moja kwa moja tabia na hulka za viongozi hao katika stahili za uoendeshaji nchi zao.

Ni kweli isiyopingika kabisa kuwa maendeleo yetu yanategemea utawala bora kiambatano ambacho kinakosekana katika nchi zetu nying za kiafrika na kwa mda mrefu mno. Mifano kadhaa aliyoitoa raisi Obama inapaswa kuwafungua macho viongozi wetu na kuanza kuyafanyia kazi maeneo yale ambayo yamekuwa yakikwamisha maendelo ya nchi zao na wananchi wao kwa ujumla.

Historia inatuambia kuwa nchi za mashariki ya mbali katika bara la Asia ambazo katika miaka ya sitini zilikuwa katika kiwango sawa cha maendeleo na nchi zetu za afrika na pengine baadhi ya nchi zetu kuzipita leo hii imebaki kuwa historia kwani zimefanikiwa kupiga hatua kubwa ya kimaendeleo katika kila Nyanja na kuziacha nchi zetu zikiendelea kulowea katika umaskini.

Raisi Obama alitolea mfano wa kusikitisha kwa nchi zetu za Afrika kama Kenya na nyinginezo ambazo zilikuwa na uchumi mkubwa kwa mtu mmoja mmoja kuliko korea kusini, Singapre, Taiwani lakini kwasasa zimepitwa vibaya. Ni kweli iliyo wazi kuwa nchi hizi hazikutumia uchawi kufika huko waliko bali ni kujipanga kiuongozi na kuweka vipaumbele vyao sawa na kwankutumia vizuri rasilimali chache walizonzao kwa manufaa ya nchi yao na wananchi wao kwa ujumla.

Matumizi mabaya ya rasilimali yamekuwa yakiendelea kukwamisha juhudi za nchi zote kujikwamua pale zilipo kwani kiasi kikubwa kimekuwa kikitumiwa katika kuimarisha dola na vyombo vyake vya usalama ili waendelea kujinufaisha wao wenyewe na kuwaacha wananchi wao wakiendelea kubaki bila mtetezi.

Ghana na Botswana zinachukuliwa kama mfano wa uwezekano wa bara hili kuendelea ikiwa tu watawala au wanasiasa waacha uzandiki katika nafsi na dhamira zao kuongoza kwa kutumia rasilimali zao walizonazo kama madini na mafuta katika kuwaletea wananchi wake maendeleo ya haraka.

Mustakhabali wa afrika uko juu ya sisi wa waafrika wenyewe ikiwa tutaamua kuyakabili matatizo yetu kwa nguvu mpya, ari mpya na kasi mpya itakayojitafsiri zaid katika matendo na sio hadaa ya kujipatia kura na kujiejengea uhalali wa kushika hatamu ya kuendelea kutafuna rasilimali za nchi kwa manufaa binafsi.

Hakuna sababu au uhalali wowote kwa magonjwa na migogoro viendelee kuvuruga maeneo mengi ya bara letu na kusababisha wananchi wetu wapoteze maisha kwa mambo ambayo viongozi wetu wameendelea kuyakumbatia. Ile dhamira ya utumishi inayopaswa kuwa msingi wa kufanya kazi kwa maslahi ya uma inapaswa ihuishwe kwa kuweka taasisi huru zinazoweza kuchochea uwajibikaji wa wale wote wanaopewa dhamana za kiuongozi.

Hakuna mtu anayetaka kuishi katika jumuiya ambapo utawala wa kisheria unageuzwa kuwa utwaala wa kikatili na hongo unaolenga katika kuwanyima wananchi wake haki za kimsingi zinazolenga katika kuwaboreshea maisha yao. Wananchi ambao kimsingi ndio nguvu kazi tegemewa ya kuziletea nchi zao maendeleo zinapaswa kuheshimiwa na kupewa fursa stahili kama sehemu muhimu ya jamii katika kuleta mageuzi kwenye nchi zetu kwa kushiriki kikamilifu katika harakati hizo.

Tunategemea nini iwapo mabunge yetu ambayo yanategemewa kuwa taasisi muhimu za kusimamia utendaji wa serikali zetu na viongozi wake yamegeuka kuwa jukwaaa la ushabiki wa kisiasa unaojikita zaidi katika kutetea na kufunika maovu ya watawala kuliko kutetea maslahi ya umma inaouwakilisha? Hulka za taasisi hizi hazileti matumaini yoyote kwa wananchi zaidi ya kuendelea kuwajengea hali ya kujiamini na kiburi watawala na serikali zao katika harakati zao za kuendelea kutafuna rasilimali za uma.

Hata misaada ya dola bilioni tatu ambazo serikali ya marekani imeahidi kuzitoa kwa kile ilichokiita kuchochea kilimo cha uzalishaji chakula kwa bara la Afrika ni wazi zitakuwa hazina tija au matokeo yoyote kama dhana nzima ya utawala bora haitapewa kipaumbele katika taasisi za kiutawala kwenye nchi zetu hizi ambazo zimeendelea kujijengea mazingira ya kuwa ombaomba kwa kipindi kirefu sasa. Zabuni katika ujenzi wa miundo mbinu ya barabara huishia mikonini mwa wajanja wachache na kuacha sekta husika zikiwa hoi kabisa.

Tunategemea nini ikiwa misaada yenye thamani ya mamilioni za dola za kimarekani zinazolenga kusadia matatizo ya kiafya kama ukimwi na kifua kikuu zanaendela kuishia kwenye matumbo ya watu wachache na kuwaacha maelfu ya wananchi wao ambao ndio nguvu kazi pekee ya kujiletea maedeleo wakiendelea kupoteza maisha kwa kukosa dawa?

Tunategemea nini ikiwa rasilimali za taifa kama madini,mafuta na mazo ya misitu yakiendelea kusafirishwa nje ya nchi kwa kushirikiana na taasisi zetu za forodha ambazo zinakosa misingi ya maadili ya utawala bora na kuzifanya nchi zetu ziendelee kuwa tegemezi? Ni kwanini vyombo hivi visimulikwe na kuwawajibisha wale watendaji wote wabovu ambao wanaongozwa na misingi ya ubinafsi kuliko ile ya maslahi ya uma.

Tunategemea nini ikiwa watu wanapewa nafasi za uongozi au utumishi kwa upendeleo na kuwaacha wenye sifa nje ya mfumo wa uendeshaji utakoasadia kuleta tija na changamoto makini katika utendaji kazi unaolenga kuwaondolea wananchi kero na hatimaye kufufua maendeleo ya nchi zetu? Tusitegemea miujiza katika maendeleo ikiwa maeneo muhimu ya kimkakati wa kisera vitaendelea kuangukia mikononi mwa watu ambao kimsingi hawana sifa au uwezo wa kuyaongoza kwa ufanisi unaotakiwa.

Haya ni baadhi ya maeneo ambayo viongozi wetu wa kiafrika hawana budi kuyatazama kwa na namna ya kipekee na kuanza kuyafanyia kazi kuliko kuamua uendelea “Kuwa sikio la kufa ambalo kamwe halisikii dawa” kwa kushindwa kutambua chanzo au sababu ya matatizo yetu na kuendelea kutafuta mchawi kwa makosa yao wenyewe.

Mungu ibariki Afrika yetu na viongozi wetu.
MAJIBU RAHISI YA WANASIASA KATIKA MATATIZO MAGUMU YATAANGIMIZA WANANCHI
Katika makala yangu ya toleo namba ….. kwenye gazeti la rai nilizungumzia ugonjwa wa wanasiasa wetu wa kiafrika hasa wa kitanzania ama kupuuzia utajiri wa kifalsafa,miongozo na maadili ya kiuongozi yaliyosisitizwa na waasisi wetu waliopata kuongoza nchi yetu na bara letu kwa ujumla. Nilijaribu kuhusisha tatizo hilo linaloonekana kuwa kubwa na ama tabia ya viongozi hao kutopenda kusoma au kupuuzia machapisho au hotuba za waasisi na wanafalsasa wetu walioandika mambo mengi mema na muhimu ambayo yanaweza kuwa ni dira muhimu katika uongozi wa uma.

Kwa leo ningependa kurejea maono na onyo alilotoa hayati baba wa taifa katika kitabu chake cha ‘Tujisahihishe’ cha mwaka 1962 mda mchache baada ya Tanzania kujipatia uhuru wake kutoka kwa waingereza na ningependa kunukuu;

“Tatizo kubwa la waafrika ni kuwa na majibu rahisi kwa matatizo makubwa”

Kwa mantiki ya mda uliopo na mambo yanavyoendeshwa kwasasa na baadhi ya viongozi wetu hatupaswi hata chembe kuhoji uwezo wa mwalimu nyerere katika kuchambua mambo na kueleza bayana hulka na mienendo ya watendaji ambao wamepewa dhamana ya kuliongoza taifa na kulivusha katika bahari ya umaskini ambao hadi sasa tiba yake imebaki kuwa ndoto za alinacha.

Katika nchi yetu ambayo wananchi wake wamekuwa wakiishi kwa matumani ya kuboreshewa maisha yao hali ya kukata tamaa inazindi kuongezeka hasa wanapopata fursa ya kusikiliza majibu ya kero zao kutoka kwa viongozi wao ambao waliwapa nafasi ya kuwaongoza. Majibu ya kisera au kimkakati kutoka kwa viongozi hao mara nyingi yamekua hayakidhi haja na kiu ya wananchi katika kuwaondelea matatizo yao.

Viongozi wetu wamekua wanaongozwa na mazoea ya ‘Funika kombe,mwanaharamu apite’ katika kero na matatizo makubwa ya kiuchumi,kijamii na kisiasa yanayowakabili wananchi wao na kuacha mizizi ya matatizo hayo ikiendelea kujichimbia katika maisha yao bila ya hata kuwa na uhakika wa kuiona kesho au kutambua hatma yao.

Ukiamua kufanya tathmini ya matatizo ambayo yamekuwa yakiendelea kuitatiza nchi yetu ijapokuwa ukiyatazama yapo ndani ya uwezo wetu ni wazi kuwa utakubaliana na hayati mwalimu nyerere katika hili la tabia ya viongozi wetu kutoyapatia majibu matatizo na kero zinaoendelea kudhoofisha nyonyo za wananchi wao ambao waliapa kwa vitabu vya mungu kuwa wangewatumikia kwa moyo na nguvu zao zote.

Ni aibu kwa nchi yetu kuendelea kushuhudia migogoro kati ya wakulima na wafugaji ambayo imefikia hatua ya kugharimu maisha na mali za watanzania wenzetu. Tumekuwa tukiamini matatizo kama hayo yangetokea katika nchi ambazo zina uhaba wa rasilimali kama ardhi na maji lakini siyo kwa nchi yetu ya Tanzania ambayo mwenyezi mungu ameibariki kwa namna ya kipekee katika hili. Majibu sahihi ya kisera na kimkakati ya matumizi sahihi ya rasilimali hizo ni wazi yamekosekana na kulifanya tatizo hili liendelee kuonekana kama ni donda ndugu.

Matatizo yanayotokana na sera ya ubinafsishaji wa rasilimali tatika sekta mbalimbali kama madini,viwanda au mashirika ya uma yameendelee kuliandama taifa letu kutokana na hulka hizo hizo za viongozi wetu kuendelea kutoka majibu katika masuala tete yanayohitaji umakini na busara katika utatuzi wake. Tatizo la mgodi wa north mara ulioendelea kutiririsha maji yenye kemikali za sumu na kuathiri maisha ya watu na viumbe hayakupaswa kutolewa maji ya kukatisha tamaa kwa kiwango kile eti ‘ mgodi ulianza uzalishaji kabla ya sheria ya mazingira haijantungwa’. Majibu kama haya kutolewa na viongozi waliopewa dhamana kubwa yanawakatisha tamaa wananchi wetu na kuwafanya wajihisi yatima katika nchi yao.

Ukijaribu kuangalia matatizo katika sekta ya elimu ambayo ni tegemeo na msingi katika ustawi na maendeleo ya taifa lolote lile utakuta sababu ni ile ile ya kutotoa majibu yanayokidhi haja ya tatizo lenyewe na kwa wakati muafaka. Matatizo ya maslahi walimu ambayo yamekuwa yakirudisha nyuma maendeleo katika sekta husika yamekuwa yakipewa majibu rahisi bila kuwepo kwa mikakati endelevu ya kuyatatua na hali imeendelea kuwa hivyo hivyo kwa matatizo ya mikopo na migomo ya mara kwa mara katika taasisi za elimu ya juu nchini.

Matatizo ya njaa na upungufu wa chakula wa kila mara yanayoendelea kuwakabili wananchi wetu yanatokana ni matokea ya kila mara ya viongozi waliopewa dhamana katika sekta husika kuendelea kubwabwaja siasa katika mambo ambayo kimsingi yanahitaji utekelezaji tu. Kauli mbiu zinazobuniwa kila mara na kyumiwa kama mtji wa kisiasa haziwezi kutuondoa katika matatizo hayo bali ni kuwa watu wa vitendo kwa kutekeleza yale yote ambayo tulishayaazmia huko nyumba.

Azimio la iringa la siasa ni kilimo lilipaswa kutiliwa mkazo na kuongezewa nguvu nguvu tu kwani lilishaainisha kila kitu lakini likabaki suala la utekelezaji tu kwaiyo hatuhitaji misamiati mipya katika suala la kuborsha kilimo na kukifanya kiwe chenye tija na hatimaye kuwaondolea wananchi wetu umaskini ambao umekuwa ukiwaandama tangu wapate uhuru.

Matatizo ya mda mrefu ya nishati ya umeme ambayo ni muhimu katika ukuaji wa sekta ya viwanda ambayo ingeweza kuchochea maendeleo katika sekta nyingine yamekuwa ni kama yanapuuzwa kwa viongozi waliopota kuongoza sekta hiyo. Imekuwa ni kawaida kwa kila waziri anayepata fursa ya kuongoza sekta hiyo kutoa ahadi na kupanga mikakati isiyotekelezeka na kuondoka bila kuacha matunda yoyote kwani wameonekana hawatambui au wanapuuzia kwa makusudi ile dhana inayojulikana kwa kizungu kama ‘forward and backward economic linkage’ ambayo ni muhimu katika ukuaji wa uchumi wa taifa lolote duniani.

Majibu ya kila mwaka ya mawaziri hao kama vile ‘Serikali imejipanga kutumia vyanzo vingine kama makaa ya mawe, upepo na mwanga wa jua katika kutatua tatizo la umeme nchini’ hayatalisaidia taifa hili kuondokana na tatizo hilo kama hakutakuwa na dhamira za dhati kushughulikia uozo uliopo katika mikataba mbalimbali ya uzalishaji umeme ambayo imekuwa haina tija kwa taifa letu.

Matatizo ya ufisadi yanayoendelea kuikumba nchi yetu ni matokea ya uundwaji sheria na kanuni ambazo zimekuwa hazina meno ya kuyakabili. Majibu ya ‘Mheshimiwa spika,uchunguzi bado unaendelea’ yanazidi kulitumbukiza taifa hili katika hatari kubwa ya kuwafanya watumishi waendelee kujikita katika mambo ya kifisadi yasiyokuwa na manufaa kwa taifa letu. Katika akili ya kawaida ukijiuliza ni kwanini wale waliofikisha nchi yetu katika mikataba mibovu kama ya Richmond hawajachukuliwa hatua hadi sasa majibu yake ni wazi kuwa hayakidhi haja.

Hakika mambo haya yanakatisha tamaa na hata kuchafua dhamira na juhudi za viongozi wengine serikalini katika kuwaletea wananchi maendeleo. Ni jambo la kukatisha tamaa kwani imekuwa ni kawaida kwa matatizo ya kisekta ambayo yako ndani ya uwezo wa watu waliopewa dhamana ya kuongoza sekta hizo kusubiri hadi viongozi wakuu wa serikali kama raisi au waziri mkuu kuyatolea tamko huku hao wakendelea kuuchapa usingizi na kubwabwaja maneno yaliyojaa kila aina ya hila na ubabaishaji. Tatizo la mapigano ya koo huko tarime au msongamano wa makontena katika bandari zetu halipaswa kusubiri hadi viongozi wakuu wan chi kama rais au waziri mkuu walitolee tamko.

Bunge kama chombo chenye wajibu wa kuishauri na kuisimamia serikali katika majukumu yake linapaswa kujitakasa upya na kuanza kutekeleza wajibu wao wa msingi. Mheshimiwa spika Samwel sita ambaye anapenda kutambulika kama mzee wa ‘KASI NA VIWANGO’ anapaswa kuitekeleza ahadi yake aliyoitoa wakati alipochaguliwa kuliongoza bunge ya kutovumilia majibu rahisi ya mawaziri katika mambo yenye maslahi ya kitaifa.

Mungu ibariki Tanzania yetu na viongozi wetu.
MITIZAMO YA AKINA IBIN BATUTA NA HULKA ZA WANASIASA WA TANZANIA YA LEO

Nchi yetu ya Tanzania tuipendayo kwa moyo wetu wote inapita katika wakati mgumu sana kisiasa na kiuchumi. Hakika ni kipindi ambacho historia itapata mengi ya kuandika kwa ajili ya vizazi vyetu vijavyo ambayo ni mategemeo ya walio wengi kuwa nchi yao itakuwa imeandaliwa vyema na kuwa sehemu salama ya kuishi huku kukiwa na misingi imara ya kuboresha maisha yatakayowawezesha kufurahia matunda ya uhuru ambao babu na bibi zao walijitoa mhanga kuyapigania.

Mtikiso wa kiuchumi unaoikumba dunia kwasasa na mawimbi ya demokrasia ambayo yameanza kuvuma kwa kasi kubwa katika nchi yetu na taasisi zake vinatupa fursa ya sisi kutafakari na kutoa mawazo yetu juu ya nini kifanywe haswa na wale watu waliopewa dhamana za uongozi katika serikali ili waweze kutekeleza wajibu wao na kutupitisha salama katika kipindi hiki kigumu na cha mpito ambacho kinahitaji hekima na uadlifu kwa kiwango kikubwa kuinusuru nchi au kizazi chochote.

Nchi yoyote ile au vizazi vyovyote katika ulimwengu huu ambao wamekua kwa namna moja au nyingine wakiidharau historia hujikuta katika wakati mgumu sana katika harakati zao za kujiletea maendeleo na hali huwa hivyo pia kwa binadamu ambao wamekuwa wakidharau maadili ya msingi ya vizazi vyao. Mila na utamaduni wetu wa kiafrika au kitanzania umekuwa ukituaminisha kwa namna ya kipekee kuwa wazee ni watu walio na busara ambao wosia au miongozo yao ni muhimu katika maendeleo yetu na kama tukifanya vinginevyo au kinyume na miongozo au mitazamo yao basi tutegemee madhara makubwa.

Nchi yetu na bara letu la Africa katika miaka ya mwanzoni mwa sitini na mwishoni mwa themanini zilipata bahati kubwa ya kuongozwa na watu wenye dhamira safi na kiu kubwa ya kuwaletea watu wake maendeleo yanayozingatia haki na usawa na yenye kukidhi haja au matakwa ya wananchi wetu. Ni viongozi ambao walikua na uadilifu mkubwa huku wakitanguliza hofu ya mungu mbele wakiamini wamepewa majukumu hayo ya kiuongozi si kwasababu ni wao pekee wenye uwezo wa kuongoza bali ni wito uliojikita katika mitazamo ya UTUMISHI ULIOTUKA ambao haulengi wao kujipatia kitu bali kuwapitia wale wananchi wanaowaongoza vitu vitakavyowawezesha kuboresha maisha yao.

Viongozi hao ambao wengi wao tayari wameshatangulia mbele ya haki walikuwa wakitumia mda wao mwingi kutafiti,kuandika,kuasa, kuonya na kufundisha yale mambo ambayo waliamini yangesaidia kujenga vizazi ambayo vinafuata maadili katika harakati zao za kujiletea maendeleo baada ya miongo kadhaa ya kutawaliwa. Sio tu kujiletea maendeleo bali kujijengea mazingira ya kuruhusu uadilifu utawale katika fikra za vizazi hivyo huku upendo ukiwa nguzo kuu ya wale wote wanaopata nafasi za kushika hatamu za ungozi wa nchi au taasisi muhimu za kiutawala ambavyo kwa pamoja ni mihimili muhimu ya kuleta na kudumisha amani.

Hakika waafrika na watanzania tumejaliwa mambo mengi muhimu ambayo tungeyatumia vyema yangeweza kutuletea maendeleo ya haraka, ya uhakika na makubwa. Sitapenda kuzungumzia utajiri wa kirasilimali tuliojaliwa nao kwani wengi wameshaandika. Leo ningependa kukumbusha wasomaji wetu utajiri wa kifalsafa,kimaadili na miongozo ya waasisi wa bara letu na taifa letu la Tanzania ambavyo kimsingi tungeamua kuviheshimu na kuvitumia tungefanikiwa kuwa na dola za kiutawala zinazoheshimu utu wa watawaliwa na kujenga misingi imara ya uwajibikaji unaofuata maadili ya kiuongozi wenye kuleta tija na unaoheshimu demokrasia ya kweli.

Ukianza kutafakari kwanini kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa kimaadili ya kiuongozi kwa wale walio katika nafasi za uongozi wa umma katika viwango vya kutisha kwa nchi zetu unaweza kurejea utangulizi wangu hapo juu kuwa inatokana na vizazi na viongozi waliopo ama kupuuzia misingi ya mawazo na maadili ya kiuongozi yaliyosisitizwa na waasisi na wazee wetu waliopata kuongoza nchi yetu na bara letu kwa ujumla.

Historia inatuambia watanzania kuwa Ibini Batuta,aliyepata kuwa mtawala na mwanaharakati katika ufalme wa morocco aliwahi kutembelea Zanzibar katika karne ya kumi na nne(14th C) katika moja ya ziara zake ndefu za kusisitiza umuhimu wa uongozi bora uliojengeka katika misingi ya kujitolea ili kuwaletea wale tunaowaongoza maendeleo yenye tija na ningependa kunukuu kipande kidogo cha maneno yaliyopo katika hotuba yake aliyoitoa wakati wa ziara yake visiwani huko ili yawe msingi wa mada hii ya leo nanukuu;

“Tutakapofariki dunia,msitutafute kwenye makaburi yaliyopakwa chokaa,
bali tutafuteni kwenye mioyo ya wale tuliowasaidia kuboresha maisha yao”

Hakika ni maneno mazito yanayopeleka ujumbe mahsusi kwa wale waliopewa dhamana za kiuongozi katika jamii na nchi zao kwa ujumla. Vizazi vilivyopo na vijavyo vinatakiwa kujifunza yale mema ambayo viongozi au watawala wao waliyasimamia ambayo waliamini kuwa yakifuatwa na kutekelezwa yanaweza kuwa nguzo muhimu za kuwaletea maendeleo.Hii ndio kazi ya historia chanya inayolenga katika kuimarisha nidhamu na imani kwa vizazi vilivyopo na kuchocchea hamu ya kujifunza au kuongeza bidii katika utendaji kazi ulio bora wa kuvuka viwango au kuweka rekodi safi za utumishi.

Nilishawahi kuandika makala katika gazeti niliyoipa kichwa cha habari “Hekima: karama iliyotoweka katika maamuzi ya viongozi na watendaji serikalini” . Nilikuwa najaribu kutazama maamuzi mbalimbali yanayofanywa na baadhi ya viongozi waliopewa dhamana za kiuongozi katika nchi yetu na kutoa angalizo la wao kubadilika kwani vuguvugu lililopo linaweza kuifikisha nchi mahali pabaya kwani wananchi wameshanza kuhoji kiwango cha maadili na uwezo wa kiakili wa viongozi wao katika kufikiri, kuamua na kutenda. Wanahoji iwapo viongozi wao wanatumia akili kufikiri na iwapo maamuzi wanayosimamia yanatambua kuwa kesho ipo? Wanahoji pia ni upi urithi wa fikra wanaowaachia vizazi vilivyopo na vijavyo?

Maswali kama hayo yamekua yanaulizwa bila kupatiwa majibu ya kutia moyo na kuwaacha watu na hasira ambazo zinaendelea kunyong’onyeza nafsi zao na kuendelea kuwakatisha tamaa.Katika maongezi yao kuna baadhi wanapendekeza vijazi vijavyo vifukue makaburi ya voingozi wao waliowatangulia na kuanza uchunguzi wa kupata uhakika wa uwezo wao wa kufikiri na kiwango cha busara kilichokuwa kinawaongoza kufikia maamuzi mbalimbali yaliyopaswa kuchukuwa muelekeo wa kutafuta mbinu za kutatua matatizo yao ili waweze anagalao kuwakumbuka kwa siku zijazo na kuacha historia itakayotukuka kwa vizazi vijavyo.

Huo unaweza kuwa msingi wa kile kilichomsukuma Ibini batuta kutoa maneno yale katika ardhi ya nchi yetu na kwa kuzingatia hulka za viongozi wetu kama mawaziri na wabunge ambao wengi wamekua wakikiuka wazi wazi na kwa makusudi misingi ya maadili ya utumishi hivyo kuleta changamoto kubwa kwetu kuwakumbusha na kuwasimamia hao waliopewa dhamana kuonyesha utumishi bora kwa yale waliyoahidi kutekeleza na kutuletea maendeleo ambayo yataacha alama isiyofutika katika mioyo yetu.

Tatizo kubwa linaloonekana kwa viongozi wetu ni ama tabia yao ya kutopenda kusoma au kupuuzia machapisho au hotuba za waasisi na wanafalsasa wetu walioandika mambo mengi mema na muhimu ambayo yanaweza kuwa ni dira muhimu katika uongozi wa uma. Ubinafsi unaonekana kuchukua nafasi kubwa katika utendaji kazi wa viongozi wa serikali zetu na hata kufikia hatua ya wao wenyewe kuanza kunyoosheana vidole na kutuhumiana na hata kuomba mungu awalaani baadhi yao.

Katika lugha rahisi viongozi wetu waliopewa dhamana ya kuongoza sekta muhimu kama za afya,elimu na kilimo na nyinginezo wanapaswa kutafakari kauli ya Ibini batuta na kujiuliza wananchi wao wataenda kuwatafuta wapi pindi watakapokua wamemaliza jukumu lao la kuongoza wizara hizo au pindi watakapokua wametangulia mbele ya haki. Ni muhimu kwa wao kuanza kutafakari juu ya kile wanachopaswa kuacha kama alama ya uongozi uliotukuka .

Kwa mfano, Je wanafunzi wa taasisi za elimu ya juu watawakumbuka mawaziri waliopata kuongoza wizara hiyo kwa lipi?? Walimu wa shule za msingi na sekondari hasa za vijijini wawakumbuke voingozi wao wenye dhamana kwa lipi?. Mahakimu halikadhalika wanaofanya kazi katika mazingira magumu ya kujenga taifa linaloheshimu sheria na haki watawakumbuka viongozi wao kwa lipi.Polisi nao ambao wamekuwa wakijitoa mhanga kulinda mali na maisha ya raia na viongozi wao watawakumbuka hao wenye dhamana kwa jambo lipi?

Wananchi walio katika maeneo ambayo rasilimali kama madini na mbuga za wanyama wananufaika vipi na wamewekewa mazingira gani yanayoweza kuwahakikishia kuwa wanafaidi matunda ya rasilimali walizojaliwa na mwenyezi mungu. Rejea kipindi cha je tutafika kilichorushwa na chanel 10 siku ya alhamisi na ujiulize, Je wananchi walio katika maeneo ya migodi kama kule tarime wanaoendelea kuathirika na kemikali zinazozalishwa katika migodi hiyo wawakumbuke wabunge na mawaziri wao kwa mema yapi? Je wananchi wawakumbuke viongozi wao kwa mikataba mibovu waliyoingia isiyo na tija yoyote kwa taifa?

Swali la msingi ambalo viongozi wetu wanapaswa kujiuliza na kutafakari ni je watanzania wawakumbuke kwa ubabaishaji wao watakapokuwa wametoka katika dhamana za uongozi au wameaga dunia? Uongozi wa kinafiki hautalipeleka taifa hili kokote na ni vyema viongozi waliopo madarakani na wale wanaoomba ridhaa ya kuongoza nchi hapa nazungumzia vyama vya upinzani wakatambua hilo. Ukitizama bunge kwasasa unaweza kupatwa kichefuchefu kwa jinsi wawakilishi wetu wanavyojifanya wamechachamaa kuwatetea wananchi wao kumbe ni hadaa tu ili wajihakikishie nafasi za kurudi tena bungeni kipindi kijacho ili waendelee kijineemesha nafsi zao kwa vipindi vijavyo. Ningependa kumalizia kwa kuwauliza viongozi wetu “Je watakapofariki dunia,tuwatafute kwenye makaburi yaliyopakwa chokaa,au kwenye mioyo yetu itakayowakumbuka kwa kutusaidia kuboresha maisha yetu”
Mungu ibariki Tanzania yetu na viongozi wetu.
HEKIMA: KARAMA ILIYOTOWEKA KATIKA MAAMUZI YA VIONGOZI NA WATENDAJI SERIKALINI

Historia ina nafasi kubwa sana katika kuendeleza ustaarabu na imani kwa vizazi vilivyopo na vijavyo.Matendo makuu ya kihistoria yaliyofanyika ktika kiwango cha juu cha busara na kwa kufuata maadili ya kazi na wakati husika nayo huwa ni chachu katika kudumisha na kuimarisha dhana ya utawala bora katika jamii husika.

Vizazi vilivyopo na vijavyo vinatakiwa kujifunza yale mema ambayo viongozi au watawala wao waliyasimamia na kuwaletea maendeleo.Hii ndio kazi ya historia chanya inayolenga katika kuimarisha nidhamu na imani kwa vizazi vilivyopo na kuchocchea hamu ya kujifunza au kuongeza bidii katika utendaji katika muelekeo au nia ya utendaji bora wa kuvuka viwango au kuweka rekodi.

Histoiria imekua ikituambia kuwa,nchi zilizoendelea kama ulaya magharabi na marekani na zinazoendelea kwa kasi kubwa kubwa kama Korea kusini,taiwani,Singapore zilifika huko kwa mchango mkubwa wa viongozi wao waliotambua umuhimu wa kuweka maslah ya taifa mbele katika kuletea jamii zao ustawi unaostahili.

Dhana ya uwajibikaji unaozingatia maadili ya utendaji kazi huwa ni chachu kubwa katika kunoa fikra za watendaji wetu na kushadihisha umuhimu wa kutumia hekima na busara katika utendaji kazi na maamuzi yanayohusu maisha ya wananchi na kutoa muongozo juu ya mustakabali ya nchi husika katika kujiletea maendeleo na kukuza ustawi wa jamii yenyewe.

Maendeleo ni hatua inayoratibiwa kwa kuzingatia vipaumbele ambayo jamii yenyewe imejiwekea katika kuwatumikia wananchi wake.katika mchakato huu viongozi au watendaji ni wadau wakubwa wenye dhamana ya kutoa muelekeo au muongozo wa mambo yapi yafanyike ambayo yataleta tija na ufanisi kwa jamii wanayoihudumia.

Utangulizi huu unatufanya sisi kuanza kutafakari kwa kina maamuzi mbalimbali yanayofanywa na viongozi wa kisiasa au watendaji serikalini katika kutimiza wajibu wao mkubwa wa kuwaletea maendeleo wananchi.

Tangu miaka ya katikati ya themanini hadi sasa,serikali yetu imekua katika kasi ya ajabu kuetekeleza maboresho mbalibali ya kisera katika sekta za kijamii na kiuchumi ambayo kwa pamoja wananchi wamekuwa wakielezwa kuwa yana lengo la kuboresha maisha yao na kuwaletea maendeleo.Viongozi hawa kimsingi wamekuwa wakiaminiwa katika kiwango kikubwa.
Mkataba kati ya watawala na watawaliwa unaofahamika kama social “contract” umekua ukitoa fursa kwa vingozi na watendaji wetu hawa kutekeleza majukumu makubwa kwa niaba yetu wananchi tukiwa na imani kuwa maslahi ya walio wengi yanazingatiwa.Maswali ya kuuliza katika namna maamuzi haya yanafanyika ni mengi na ambayo mara nyingi yamekua yakikosa majibu thabiti na ya kuridhisha kutoka kwa wale waliopewa dhamana.

Ubinafishaji wa mali za uma na rasilimali za kitaifa ni sera mbayo imekuwa ikipewa msukumo mkumo katika serikali ya awamu ya tatu na yeyote aliyeonekana kupinga sera hiyo amekua akionekana kama adui mkubwa wa maendeleo na anayepaswa kuhukumiwa kwa kesi ya kuhujumu harakati za kitaifa za ukombozi wa kiuchumi.

Wananchi wengi kwasas hawaonekani kuogopa kuhoji maamuzi ya watendai na viongozi wao.Wananchi wanazidi kutambua kuwa wana mchango na jukumu kubwa katika kuratibu na kusimamia mambo yenye muelekeo wa kukomboa mustakabali wa taifa lao.Wananchi wengi wameanza kupinga sera ya ubinafsishaji ambao kimsingi imekua ikitekelezwa kwa ubabaishaji wa hali ya juu na kuendelea kugharimu maisha ya wananchi wazawa.

Vijana ambao wako wengi nao wanazidi kusimama imara bila woga na kutoa wasiwasi wao juu ya hekima zinazowaongoza viongozi wao katika kufikia maamuzi mbali yanayohusu maisha yao katika nchi yao ambayo wanazidi kutambua kuwa nao ni wadau muhimu na sio watawala au viongozi waliopewa jukumu la kuwaongoza.

Ukiona wanajamii wananza kuhoji uwezo wa kufikiri wa viongozi wao basi ujue kua mambo si shwari tena na jitihada zinapaswa kufanyika kuondoa hatari hii ya kupoteza imani kwa viongozi na watendaji ambao wana jukumu la kufanya maamuzi na kusimamia maamuzi hayo kwa manufaa ya wanajamii wanaowaongoza.
Ukitembea katika maskani za vijana na barabarani utasikia wananchi wanahoji,Hivi hawa viongozi wetu wanatumia akili kufikiri?Hivi maamuzi wanayosimamia yanatambua kuwa kesho ipo? Hivi vizazi vijavyo vijifunze yapi mema kutoka kwao?Ni upi urithi wa fikra wanaowaachia vizazi vilivyopo na vijavyo?Je,na sisi tuige ubabaishaji kama wao katika mamuzi?

Maswali kama hayo yamekua yanaulizwa bila majibu ya kutia moyo na kuwaacha watu na hasira ambazo ni wazi zinawakatisha tamaa.Katika maongezi yao kuna baadhi wanapendekeza vijazi vijavyo vifukue makaburi ya voingozi wao waliowatangulia na kuanza uchunguzi wa kupata uhakika wa uwezo wao wa kufikiri na kiwango cha busara kilichokuwa kinawaongoza kufikia maamuzi.Hapa namkumbuka mwanasayansi mmoja wa kimarekani aliyetoa matokea ya utafiti kuhusu uwezo wa akili kati ya watu weusi na weupe.Vijana wetu wanasema utafiti huo ulikua unawalenga viongozi wa na watendaji wa serikali za kiafrika hususani Tanzania.

Sera ya ubinafsishaji inayopigiwa chapuo na benki ya dunia na shirika la kimataifa la fedha imethibitika kuwa haina tija katika kuwaletea wananchi wetu maisha bora na badala yake imeonekana ni kama msumari wa mwisho unaopigiliwa katika makaburi ya nchi maskini duniani na zile zinazoendelea ikiwemo Tanzania ambayo maamuzi mengi ya viongozi wake yameigharimu na kuendelea kugharimu ustawi wa wananchi wake.

Katika yote hayo hekima inaonekana kukosekana katika kila mambo au maamuzi mengi yanayofanywa na viongozi wetu.Vizazi vijavyo ni kama vitabaki bila mwalimu wa kujifunza kutoka kwao na kuendelea kuweweseka na kujikuta wakitumbukia katika shimo la taka lilikosa staha ya kuchammbua zuri na baya la kuhifadhi.

Viongozi wetu wamekuwa wakihudhuria warsha za kimataifa za kimkakati kila kukicha lakini matunda yake yamekua ni kama ndoto.Viongozi wamekua wanashiriki kikamilifu katika maandalizi ya sera na mikakati ya kiutekelezaji ya kibabaishaji lakini baadae wamekua wakiikana na kuonea aibu kuwa sehemu ya hiyo mikakati baada ya licha ya kutambua kila awali kuwa haina tija.
Wananchi wanakosa subira ya kuhoji iwapo viongozi wao wanatumia vilevi kabla ya kushiriki katika michakato mbalimbali ya upangaji sera na kufanya maamuzi yenye malengo ya kuinua maisha ya watu wake.Mifano katika hili ni mingi sana naya kukatisha tamaa.Kuna msemo wa siku nyingi unaosema kuwa ‘Ukibebwa na wewe ubebeke au ujishikile’.Msemo huu pia amekea akiutumia rais kikwete katika baadahi ya hotuba zake kwa wananchi.

Nchi wahisani wamekua wakijitahidi kutoa misaada mbalimbali za kimaendeleo tangu uhuru kwa nia moja kubwa ya kuboresha maisha ya wananchi wetu.Matokeo ya miradi ambayo imekua ikifadhiliwa na wenzetu hawa ni kama hayapo.Ukifika wilaya ya mbarali utasikia hadithi za kusikitisha katika ule mradi wa umwagiliaji uliofadhiliwa na serikali ya wachina kama zawadi chini ya utawala wa Mao Tse tung mikana ya sitini.

Mfereji huo mkubwa na wa kisasa uliokua matumaini kwa wananchi wa eneo husika sasa unabaki kuwa ndoto na chanzo cha manungu’niko kwa wakazi wa eneo hilo.Serikali mara zote imekua ikitoa kisingizio cha kukosa fedha za uendeshaji miradi na kufikia maamuzi ya kubinfsiha.Mradi huu wa umwagiliaji ulikua unastahili usimamizi na sio mtaji kama wengi wanavyopsawa kuamini.Katika mazingira haya ndo yanayowapelekea wananchi kuhoji busara na hekima inayowaongoza viongozi wao katika kufikia uamuzi wa kubinafsisha mradi kama huu wa umwagiliaji.

Ni wazi kuwa viongozi hawa wanatambua kuwa asilimia kubwa ya wakazi wa eneo hili huetegemea kililmo cha mpunga katika kuendesha maisha yao.Kubinafsisha mfereji huo kwa mtu binafsi ni kuwasaliti wananchi ambao kimsingi wanapaswa kunufaika nao.Hivi sasa aliyekabidhiwa mashamba hayo na mfereji huo mkubwa uliofadhiliwa na serikali ya watu wa china anawakodoshia wazawa.Hakika huu ni unyonyaji ulio dhahiri kwa wananchi.

Ni hekima gani iliyoyumika kuubinafsisha mradi huu kwa mtu mmohja na kuwaacha maelfu ya wananchi wa maeneo hayo watumwa na wasio matumaini katika kuboresha maisha yao wakitegemea kilimo ambacho ni wazi kuwa ndio mkombozi wa wakazi wa eneo hilo?Ni wazi kuwa viongozi kwasasa wanatambua madudu katika utekelezaji wa maamuzi hayo,lakini suala kubwa lililobaki ni,nani amfunge paka kengele katika kubadili maamuzi hayo dhalimu kwa wananchi wa maeneo hayo.

Rasilimali mbalimbali za kitaifa zimekua zikipotea kutokana na maamuzi mbalimbali ya viongozi wetu yanayoweka hekima kando kwa ajili ya maslahi binafsi.Vizazi vyetu vijufunze yapi mema katika yote haya ya kibabaishaji yanayoendelea kufanywa na viongozi.Kubinafisha misitu,migodi kwa mikataba isiyo na kikomo au ya kibabashaji,je ilihusisha hekima gani katika kufikia huko?Hizi ni changamoto ambazo zinapaswa kufanyiwa kazi na viongozi wetu badala ya kuzifanya za kiitikadi ili kuweka mazingira kwa vizazi vilivyopo na vijavyo kurithi mema kwa maslahi ya taifa letu.
SAKATA LA EPA, NI JARIBIO KWA SERIKALI INAYOJIGAMMBA KUFUATA NA KUHESHIMU UTAWALA WA SHERIA.

Katika mambo ambayo watanzania tumekua tukijigamba na kutembea vifua mbele ni AMANI
iliyotawala nchini tangu tulipopata uhuru karibu miongo minne na nusu iliyopita..Nchi yetu imetokea kua kimbilio la wageni kutoka nchi majirani amani kwao imekua ni ndoto kutokana na vita vya wenyewe kwa wenyewe au misuguano ya kimakundi au kimatabaka kati ya watawala na wananchi wao au kati ya makundi mbalimbali ya kijamii hasa ya wale walionancho na wasionacho na wale wasiotarajia kuwa nacho.
Proffesor Shivji amekuwa akiyagawa matabaka hayo katika makundi matatu, Walalahai, walalaheri na walalahoi. Sina haja ya kuingia kwa undani katika uahalisia wa maisha ya mtanzania wa kawaida yalivvyo kwani takwimu na mazingira tunayoishi yanajitosheleza kutoa mwanga halisi wa mambo yalivyo na yanavyoendelea kuwa kila kukicha.

Nadhani ni busara kwa watawal wetu kutambua maswahibu yanayowakumba wenzetu wa nchi za jirani mengi yalichangiwa kwa naman mifumo ya siasa katika siasa katika nchi zao zilivyobuniwa na kuendeshwa na namana mifumo ya kutetetea haki za wananchi zinavyoendeshwa.
Jaji mkuu mstaafu Barnabas Samatta alishawahi gusia juu ya umuhimu wa vyombo vya sheria hasa mahakama katika kudumisha amani ya nchi husika kwa kuweka bayana kua...nanukuu "Iwapo jamii itapoteza imani kwa mahakama zetu ndio itakua mwanzo wa kupoteza amani nchini" Inawezekana ikaonekana ni sentensi fupi na iliyozoeleka lakini suala linabaki kua ni jitihada zipi zimefanyika katika kunusuru hali hiyo isitokee???

Tunafanya nini ili kuhakikisha wananchi wetu hasa wale waliokata tamaa hawapotezi imani kwa vyombo vyetu hivi ambavyo ni mhimili muhimu katika utawala wa kidemokrasia na wenye kuheshimu haki za binadamu?Serikali yetu inaziwezesha vipi vyombo hivi tukufu katika kutekeleza majukumu yake matakatifu ya kugawa haki sawa kwa wote?

Nimeamua kurejea kauli ile kwasasa wakati malalamiko yanazidi kua mengi kufuata kigugumizi cha serikali kuwafgikisha wale wahuskia wote katika kashfa ya ufisadi uliofanywa kwenye akaunti ya madeni ya nje(EPA).Wananchi wamepoteza imani kwa serikali yao wakirejea maneno yale yale ya wanyonge siku zote ndio wamekua wakiona upanga wa nguvu za dola na pia menno za mahakama katika utoaji wa haki.

Siku za hivi karibuni,wanasiasa na wananchi wa kawaida wamekua wakishinikiza wafungwa wote walio katika magereza mbali mbali nchini waachiwe huru ikiwa mafisadi waliohusika katika wizi wa mabilioni ya katika benki kuu wachukuliwe hatua stahili.Wakati changamoto hii ikiwa bado haijapata ufumbuzi stahili wananchi wanaanza kuzua wasiwasi mpya kua waliofikishwa mahamakani sio wahusika wakuu katika hilo.Sidhani ni busara kuingia kwa undani katika hilo ila naiachia mahakama jukumu iliyokabidhiwa kwa mujibu wa sheria kuhakikisha haki inatendeka.

Changamoto ni nyingi katika kufuata na kuheshimu utawala wa sheria bila kuangalia historia,cheo au hadhi ya mtu aliyelketwa mbele ya sheria.Kumekua na ucheleweshaji wa kesi katika kiwango cha kukatisha tamaa.Sina nia ya kubeza kila jema linalofanywa na na mahakama zetu na serikali yetu ila ni katika kuleta changamoto kwenye mchakato wa wadau kuelekea kwenye ujenzi wa jamii wenye kuheshimu haki za wananchi wenzetu ni lazima tubuni mfumo imara utakaoleta tija katika kutafuta haki.

Haiingii akilini kwa mtanzania yoyoyote yule kuona nduguye anasota rumande kwa miaka mingi bila shauri lake kupelekwa katika vyombo husika wakati mafisadi na watu wenye hadhi zao wakiwahishwa mahamakamani na misururu mirefu chini ya ulinzi mkali kama msafara wa kiongozi mkuu wa nchi.

Siku zote binadamu amekua na tabia ya kujaribu njia mbadala pale anapoona nia na mitazamo yao haiendi sawa na kama walivyotaraji....vitendo vya kuchoma vibaka moto ni kielelezo kirahisi cha kuelezea kuchoshwa na ufanisi wa baadhi ya taasisi au asasi zilizokabidhiwa majukumu ya kusimamia mambo kama hayo....Kwanini raia ambaye amechoshwa na tabia ya jambazi sugu au vibaka wazoefu asiamue kuchukua sheria mkononi wakati kila wanapopoleka malalamiko yao kwenye vyombo husika,hakuna maamuzi ambayo yataonekana kukidhi kero za walalamikaji!

Sakata la watuhumiwa wa EPA kama serikali na taasisi zake hazitakua makini linaweza kubadil hali ya upepo wa uvumilivu wa wananchi na kuenda mbali zaidi na kuhoji uhalali wa uwepo wa serikali yao ambayo waliiamini na kuipa jukumu la kua msimamizi wa rasilimali zao kwa faida yao wenyewe na kwa ajili ya vizazi vijavyo.
Kwa kumalizia napenda kutoa changamoto kwa serikali yetu kua makini katika kusimamia na kutatua kero za wananchi wake ili waendelee kua tayari katika kushiriki kikamilifu utekelezaji wa mipango ya maendeleo yao.

Nina imani kubwa na serikali ya mheshimiwa JK kwahiyo chondechonde watendaji msimwangushe katika nia yake njema ya kujenga nchi moja inayoheshimu haki na yenye kuweka mazingira ya kila mmoja kufaidi matunda ya uhuru.

Ni ukweli ulio wazi kua ubabe wa baadhi ya watendaji hauna nafasi kwasasa kwani mwisho wake hautupi matumaini yoyote mazuri.Mfano mzuri tunao kwa migomo inayoendelea kwa wanafunzi wa elimu ya juu,hii ni ishara ya kuchoshwa na ubabaishaji wa baadhi ya watendaji.

Nadhani busara itatendeka katika kutoa haki kwa wanafunzi waliogoma wakishinikiza serikali iyaangalia maombi yao kwa jicho la huruma na sio kukurupuka kutoa adhabu kwa wale ambao siku zote wamekua wakitolewa kafara kama vinara wa migomo ilhali kila mmoja anajua wazi kuwa wao ni wawakilishi wa madai ya msingi yanayotolewa na wenzao wengi ambao wamekua wanataabika katika kutetea haki zao.

Watanzania hawategemei vijana hawa waitwe wahuni kama ambayo waziri alishawahi kuwaita wanafunzi hao wanaharakati wa haki katika taasisi kama chuo kikuu cha Dar Es Salaam.Napata hofu kuwa kama waziri anasema wale wanaogoma katika kutetea haki zao na za wenzao ni wahuni,tafsiri itakayojengeka miongoni mwa watanzania ni kua hata viongozi wetu ambao wamepita chuoni hapo ni wahuni.

Mungu ibariki Tanzania,mungu ibariki Africa.

Thursday, October 09, 2008

Kikwete chukua tahadhari wananchi wanakuasi

Uasi katika kamusi ya Kiswahili umepewa tafsiri ya tendo la uvunjaji wa kanuni, sheria au amri na pia imeelezwa kuwa ni tendo lolote la uhalifu unaolenga kuvuruga amani katika nchi au jamii husika. Nimekua nikitafakari matukio ya hivi karibuni ya wananchi kukaidi amri au maagaizo ya serikali bila uoga wowote na ujasiri huo umekua ukiongezeka kwa kasi ya ajabu.

Mijadala mikali imekua ikiendelea kuibuka kila kukicha kupinga hoja au maelekezo yanayotolewa na watendaji wakuu wa serikali. Kauli zenye jazba, hamaki na zilizosheheni matusi ya nguoni zimekua zikielekezwa kwa watu muhimu waliopewa dhamana ya kuboresha maisha ya Watanzania maskini ambao hupigana usiku na mchana kutafuta kipato kilicho chini ya wastani wa dola moja ili kuweza kujikimu maisha yao na watoto wao.

Si lengo langu kujitumbukiza katika mijadala hiyo, bali kutaka kufikisha ujumbe kwa watawala wetu hasa Rais ambaye ndo nahodha wa meli yetu iitwayo ‘MV Tanzania’. Ujumbe wa kwanza ni kuwa watawala watambue kwamba Watanzania wa sasa si wale wa miaka ishirini iliyopita waliokuwa wanatambulika kama watu wa ndiyo mzee!

Sio wale waliokuwa wanadhani kumpinga kiongozi wao ni utovu wa nidhamu!Bali sasa wanajua ni wajibu na haki yao ya msingi kuhoji pale ambapo wanaona mambo hayaendi sawa sawia.
Mfululizo wa migomo unaondela katika nchi hii si jambo jema na la kutia matumaini bali ingetosha kuwakosesha usingizi watu waliopewa dhamana kusimamia utekelezaji katika idara au sekta husika ‘Respective portifolio’. Nilianza kuingiwa hofu pale wanafunzi wa shule za msingi na sekondari walipoamua kujitokeza barabarani kupinga ongezeko la nauli huku wakiwa wamebeba mabongo yenye ujumbe wa kejeli kwa viongozi waandamizi wa serikali yetu.

Wafanyakazi katika kila sekta nao hawakamatiki. Inauma sana na kutia mashaka pale unapoona wafanyakazi wa sekta ya afya kila siku malalamiko na vitisho vya kugoma haviishi. Wagonjwa wanaishi kwa hofu kuu na kukata tamaa kwani hawajui ni lini hawa watu wataweka vitendea kazi vyao chini na kusababibisha madhara makubwa.

Nazidi kuwaonea huruma wale ndugu zangu wanaougua shinikizo la damu kwani utulivu wa fikra ambao ni tiba muhimu ni kama haupo katika mazingira hayo ya utoaji huduma. Wakina mama wajawazito nao hofu kila siku inazidi kutanda kwani hawajui kama viumbe vyao walivyoteseka kuvibeba katika matumbo yao wataviona vikiwa hai kwani uhakika wa huduma umetowaka kwa sasa.

Katika utangulizi wa makala hii niliieleza nini maana ya uasi. Neno hili kama nilivyosema limekuwa likihusishwa na uovu unaolenga kuleta machafuko au hali ya vurugu kwa jamii husika.Nikitafakari kwa undani naona kuna mantiki kubwa katika kitendo hiki cha kuasi kama kitakuwa na lengo la kuleta mabadiliko kwenye jamii yenyewe.Natamani sana wananchi waendelee kuasi kwa lengo kuu na la dhati la kubadilisha maisha yao ambayo kwa sasa wanaona na kudai yanaharibiwa au kuchafuliwa na watu waliowapa dhamana ya kuwaongoza.

Kila kona ukipita utasikia usemi huu “Hivi hii nchi ina viongozi kweli” kutoka kwa raia wa kawaida ambao awali hakuna mtu angedhani watu wenye tabaka la chini na walalahoi wangeweza kupata ujasiri wa kuhoji kwa kiwango hicho cha kejeli. Hofu za watu hawa dhidi ya watawala imetoweka, imani waliyokuwa nayo awali nayo imekalia kuti kavu hakika hakuna maneno mbadala ya kusema zaidi ya “Nahodha wetu Kikwete shika usukani wako kwa makini”.

Nilishawahi kuandika makala moja yenye kichwa cha habari “Mheshiwa raisi ukiamua unaweza” na leo ningependa kukuomba urejee makala ile kama ulipata bahati ya kuisoma au hata kuhadithiwa. Nchi hii mheshimiwa rais ni changa sana na watu wa kuitoa hapa ilipo ni Watanzania wenyewe kuchapa kazi bila kuchoka na kwa kwa moyo mkuu na sio wahisani kama ambavyo viongozi wetu wengi wamekuwa wakihubiri kila kukicha.

Serikali imeenda mpango mkubwa kukuza kilimo lakini napatwa na wasiwasi na kasi ya madai ya wadau muhimu katika sekta ya usafiri kama wa reli kutishia kugoma kila siku. Je, mazao yatakayozalishwa yatasafirishwa vipi ikiwa usafiri wa anga umekua unabaki kua historia kwa wakulima wetu wa vijijini?Je, mpango mkubwa wakukuza elimu ya msingi na serikali utafanikiwa vipi ikiwa kila siku walimu wanagoma kutishia kuingia madarasani? Elimu bora itapatikana vipi ikiwa tatizo sugu la usafiri kwa wanafunzi halitapatiwa ufumbuzi wa kudumu ili kuwaondelea adha ya hofu wakati wa asubuhi na jioni wakielekea na kutoka mashuleni?

Mheshimiwa raisi kikwete wananchi hawa si wavunjaji wa makusudi wa sheria wala si wendawazimu wa kutaka kupoteza mda pasipo kuchapa kazi bali wanataka sikio litakalosikia na kuwahakikishia kuyapa madai yao uzito unaostahili ili nao wajione ni sehemu ya nchi hii kwani wamekuwa wakivuja jasho jingi ili kuwahudumia wapiga kura wako ambaomda si mrefu utawarudua tena kuwaomba ridhaa ya kuwaongoza.

Sidhani kama itakuwa ni busara pale mwaka 2010 utakaporudi na kuwauliza kwamba wanavaa viatu namba ngapi wakati vipimo ulishavichukua tangu mwaka 2005! Maandamano ya wazee wastaafu wa iliyokua Jumuiya ya Afrika Mashariki ya kutaka kukuona wewe binafsi ni ishara tosha ya wewe kutambua wasaidizi wako wamepoteza imani kwa wananchi wanaowahudumia. Huo si uasi bali ni chachu ya mabadiliko ya kiutendaji.Naamini wewe ukiaamua unaweza liwe hata kesho na kero hiyo itoweke machoni kwetu. Si busara katika hali ya kawaida kuona wazee wakilia machozi huku wakijigalagaza chini kudai haki yao ya utumishi uliotutaka kwa nchi hii kwa kitambo chote hicho.

Nimekuwa najiuliza iweje watumishi wengine walio katika ngazi za utendajii wanapogeuka mbogo kudai marejesho ya fedha wanazotumia wanapokwenda safari au kucheleweshwa kupewe japo posho zao! Kwa nini wafanye hivi wakati wanakwamisha malipo halali ya wastaafu niliowazungumzia hapo juu ama kutofanikisha maenedeleo ya nchi ambayo inawapa mishahara na nafasi ya kuomba posho na safari kila kukicha?

Kwa nini walimu, madaktari na wengineo wabaki kugoma ili kupata haki yao ya kupandishiwa mishahara huku hali ya maisha ikifahamika wazi kuwa imepanda? Je, taifa hili linatoa haki nyingi kwa kundi la akina ninyi mheshimiwa Rais na kupora haki za watu wa chini ambao wanakilishwa na walimu, madaktari na wafanyakazi wa sekta nyingine?

Wahenga walishasema kuwa, ‘mdharau mwiba mguu huota tende!’ Kwa mantiki hii hatuna budi kuchukua tahadhari kukabiliana na hili vuguvugu la migomo, manung’uniko na kila aina ya ukatishwaji tamaa visigeuke kua vyanzo vya vuruga katika taifa letu ambalo limekua likisifiwa kila mara kwa kudumisha amani tangu uhuru. Kuna usemi mmoja ambao umekuwa ukitawala sana kwa watu wanaopenda kunywa vilevi kuwa “Mpe maskini kileo asahau shida zake”. Mantiki ya usemi huu iko wazi sana na ni wajibu wa viongozi wetu kuufanyia kazi.

Wananchi hawa wanaoasi kila kukicha, hawataki madaraka ya kuongoza nchi hii au nafasi za kisiasa; bali ni haki zao na madai yao ya msingi kusikilizwa na sikio lenye huruma na kuwaondoa katika adha ya maisha haya ya mateso na shida wakati wanadai haki zao. Wanafunzi, walimu, madaktari, wauguzi na wafanyakazi wengine katika sekta za usafirishaji hawana la zaidi mheshimiwa rais zaidi ya kutatuliwa kero zao za madai.

Ili tuijenge nchi hii inapaswa kila mtu atimize wajibu wake katika kila eneo alipo. Hali hii itasaidia kuharakisha jitihada za kuiondoa nchi yetu katika lundo la kero zisizokwisha. Ni wazi kua haya hayatafanikiwa ikiwa kila siku watu wako barabarani wamebeba mabango ya kilio katika kila kazi wanayofanya na kuwakatisha tamaa hata wale wanaojiandaa kuingika katika utumishi wa aina hiyo.

Ukipita vyuo vya Ualimu na Vyuo Vikuu ambapo walimu wanaandaliwa utajua kuwa hali si nzuri na haileti matumaini yoyote na tija katika utendaji kazi. Walimu wanafunzi wamekata tamaa, madaktari wanafunzi wamekata tamaa katika kiwango cha kutisha kiasi kwamba wanajuta kwa nini wamejitumbukiza katika fani ambazo badala ya kuwalipa neema inawalipa kero kuu inayowafanya kujikondoea kama vile wanaishi bila kula au kunywa.

Hii nchi ni yetu sote ila tunatofautiana katika majukumu ya kiutendaji kwa hiyo sioni sababu kwa nini wale waliopewa dhamana ya kuwatimizia mahitaji muhimu na ya msingi wale walio nje washidwe kufanya hivyo kwa hiyo zifanyike jitihada za makusudi kufanyia kazi kwa kasi hizi kero za wananchi ili kuondoa fikra zalizojengeka miongoni mwa Watanzania walio wengi kuwa “nchi hii inajengwa na wenye moyo na kuliwa na wenye meno”. Mungu ibariki Tanzania.
TUNAJUA UNA DHAMIRA YA DHATI MHESHIMIWA RAIS; TUNASUBIRI UWEZO WAKO UTAMALAKI
Mheshimiwa Rais,ni miaka miwili na nusu sasa imepita tangu ukamate madaraka ya juu katika nchi hii changa iliyojaliwa kila aina ya rasilimali adhimu lakini bado inasota kwenye dimbwi kuu la umaskini.Nafarijika kua yaliyojiri hivi karibuni yamekupa jawabu ambalo lilikua wazi ulipoulizwa kwanini Tanzania ni nchi maskini wakati ina kila rasilimali muhimu za kuchochea maendeleo kwa kasi na nguvu kubwa.Hilo la BOT ni moja tu mheshimiwa yanayoweza kueleza kwanini juhudi zako na zetu sote hazizai na hazionyeshi matumaini yoyote ya kuzaa matunda.

Mheshimiwa Rais, ni mengi yalisemwa juu yako baada ya kupitishwa na chama chako katika mchakato uliovuta hisia za watu wengi huku tukishuhudia mijadala iliyojengwa katika misingi ya ubaguzi na kishabiki ya urangi, ukabila na uwenzetu. Kuna ambao hatukua na hofu juu ya uwezo wako,dhamira yako na utashi wako katika kutumikia umma huu wa watanzania walioanza kupoteza matumaini baada ya kipindi kirefu cha kuteseka.Hakika uteuzi wako ni kama vile ulihuisha nuru ya mafanikio kwa watanzania kwa kiwango cha juu sana.

Mheshimiwa Rais, wengine walikuhukumu kwa haiba yako!!!eti sura yako nzuri haina mashiko katika siasa za mikikimiki za kibongo!!!Hakika hii ilikua pigo kubwa katika mapambano ya kifikra kwa watanzania.Nikapiga moyo konde kwa kusema mbona hata Clinton alikua na haiba ya kuvutia lakini akaacha historia ya kiutawala licha ya kuandamwa na misukosuko mingi ya vimwana katika ikulu ya marekani!!!Fikra kama hizo hakika hazikua na maana kwa watu wenye akili timamu.

Mheshimiwa Rais, Hotuba yako ya December 30 2005 wakati unazindua bunge ilikua ni hatua muhimu ya kubadili mitazamo hasi juu yako.Hakika matumaini yalihuishwa kwetu sote tuliokua na imani juu yako japo tukikatishwa tamaa na baadhi ya shutuma na fununu zilizoandama uteuzi wako na wasaidizi wako katika kutimiza ilani ya chama chako iliyofanikiwa kushinda kwa mithili ya kishindo cha 'tsunami' kama tulivyoshuhudia wote.

Mheshimiwa Rais, naomba katika makala hii nikufananishe na mpasha mwaidha wa timu(team coach). Wewe ni mtu wa muhimu sana katika kusoma uwezo wa timu yako na kufanya mabadiliko kadha wa kadha ili kujihakikishia ushindi wa timu yako. Haiwezekani kamwe mapenzi yako juu ya wachezaji fulani kukakufanya uache kufanya mabadiliko kwa hofu ya kuharibu uhusiano wako na wachezaji wako ambayo matokeo yake ni wazi kuwa unaweza kupoteza mechi na pia kupoteza imani ya mashabiki wako ambao siku zote huwa na shauku ya kocha wa timu yao kuandaa kikosi cha ushindi ambacho daima kitawaletea furaha.

Mheshimiwa Rais,kauli yako uliyoitoa Dodoma wakati wa kuhutubia bunge bado iko vichwani mwa watanzania wengi na ninadiriki kusema ilikua ni kauli ambayo ilifanya uma wa kitanzania kusema kua "Sasa kazi imeanza".Mimi binafsi nilikua nina shauku sana ya kuona mambo makubwa yakitokea siku za usoni.

Mheshimiwa Rais, je unakumbuka kauli hii "URAIS WANGU SIO WA UBIA NA MTU". Hii ni kauli nzito iliyojengwa katika umakini na udhati mkuu uliyoitoa mbele ya chombo tukufu cha kutunga sheria ambacho ni cha wawakilishi wa watanzania waliokupigia kura huku jua likiwawakia utosini mwao.Ni kweli kabisa wewe ndo mwenye dhamana ya kuongoza timu yako bila kushawishiwa vinginevyo na yoyote yule ambaye ataonyesha kutimiza matakwa yake binafsi kinyume na matarajio ya wengi ambao ni watanzania wenzako.

Mheshimiwa Rais, hivi umeshagundua kua ndani ya timu yako au jeshi lako kuna "Mamluki" wanaofifisha jitihada zako? Nadhani bado utakua unamkumbuka mwanafalsafa mmoja kwa jina la NICOLLO MACHIAVEL.Huyu mtu alipinga sana matumizi ya wanajeshi mamluki au wa kukodi akiamini kabisa hawana uchungu wa kupigania nchi yao kwa dhati kwani wanaongozwa na tamaa ya pesa zaidi kuliko uzalendo.

Mheshimiwa Rais, je umeshafanikiwa kuwatambua watu wa aina aliyoisema mwanafalsafa huyo katika timu yako au jeshi lako ambalo aliyekutangalia alilibatiza jina la askari wa miavuli? Je kama bado, ni ipi nafasi yetu kuwaanika watu hao ili hatua za dhati uzichukue???Naamini hutawabania kama ilivyo kwa orodha ya wafanyabiashara wa unga na majambazi ambao watanzania wenzako waliamua kukuletea kwa nia njema kabisa lakini hadi sasa hatujashuhudia lolote lile au ndo mambo ya subira huvuta heri!!!

Mheshimiwa Rais,hatua za haraka ulizochukua baada ya kuuawa kwa watanzania wenzetu wafanyabiashara wa mahenge kutoka mkoani Morogoro ilikua ni kama mwanzo wa mapambano ya ukweli na dhati dhidi ya ubabaishaji wa watumishi wengi wa umma.Sitaki kuamini na kusema ile ilikua ni nguvu ya soda au uamuzi ule ulifanyika kwa vile ulikua unahusisha dagaa wadogo ambao wasingeweza kutia doa serikali yako kuu iliyoingia na ahadi kibao za matumaini .Hatujakata tamaa bado tunasubiri pengine tutasawazisha kwenye dakika za majeruhi ukizingatia hapa bado tuko mapumziko(Half time).

Mheshimiwa Rais, nilishasema hapo awali na ninarudia tena "Ukiamua uwezo wako utatamalaki". Wewe umepewa mamlaka makubwa sana mheshimiwa rais ili uweze kudhibiti utovu wa nidhamu kwa wasaidizi na wachezaji wako na sioni sababu kwanini ushindwe kutimiza matumaini yetu na matarajio tuliyonayo kwako!!Hili la BALALI ni moja tu ambalo nathubutu kusema ni kama vile umepapasa tu na bado hujaamua kushika. Hakika ukiamua, Tanzania yenye neema, haki na usawa katika mgawanyo wa rasilimali za nchi yetu inawezekana.

Mheshimiwa Rais, hivi unamfahamu huyu jemedari mkuu anajiita "JEETU PATEL".Kama nimekosea herufi za jina lake naomba uniwie radhi kwani huwa mara nyingi sipendi kusoma habari zake kwani zimekua zikinichafua roho na kunikatisha tamaa ya kuishi katika nchi hii hiyo tuliyozoeleshwa kuamini kua imejengwa katika misingi ya usawa na haki. Hivi yeye ni nani katika nchi hii asiyefikiwa na mikono mirefu ya dola na sheria ambayo ina uwezo wa kuwafikia wamachinga na vibaka wadogo waliotapakaa nchi nzima!!Au unataka tuamini kua huyu ni mtume wa mwenyezi mungu asiyepaswa kuhojiwa lolote na mamlaka za kidunia!! Jibu hapa nadhani ni hapana na pengine wewe kwa kimoyomoyo unasema "Dawa yake iko jikoni inachemka". Tunayo imani na wewe mkuu.

Mheshimiwa Rais, kauli yako uliyoitoa wakati wa hotuba yako ya kufunga mwezi wa Januari 2008 ya kutaka kutenganisha siasa na biashara ni ishara ya tumaini jipya linaloendeleza na kudhifirisha umakini wako kiutendaji .Je nia hiyo uliipata siku moja kabla ya kutoa hotuba au ilikua fikrani mwako tangu zamani??Naomba univumilie sana mheshimiwa rais kwa maswali yangu ya uchokozi.Sio utovu wa nidhamu bali ni shauku ya kutaka kujua mambo hasa yanayohusu nchi yangu na viongozi wangu waliokubali kutoa kiasi kidogo cha fedha kugharamia elimu yangu inayonipa ujasiri japo wa kuhoji haya ambayo vinginevyo nisingekua na uwezo wa kuhoji.

Mheshimiwa Rais, mimi nilidhani kabisa kua kauli hii ungeanza kuitekeleza ndani ya chama chako katika uchaguzi mkuu uliopita siku si nyingi ambao kwa hakika unaandaa mazingira ya watu hao kutembea vifua mbele katila ulingo wa siasa za nchini mwetu.Hii ni vita kuu uliyoitangaza na hauna budi kuipigana hadi mwisho wake na kama utaitekeleza kwa vitendo utakua hujachelewa hata kidogo na watanzania wote bila shaka watakua nyuma yako na kukuunga mkono katika jambo hili nyeti.

Mheshimiwa Rais, nafarijika sana na kauli hii ya kutenganisha biashara na siasa kwani imekuja wakati nikiwa bado natafakari kwa kina kauli kama hiyo iliyotolewa na kijana ambaye nadiriki kusema kua alionyesha kiwango cha juu cha umakini na uadilifu katika siasa na utumishi wa uma.Hili nalo nitaliandalia muda wake maalumu ili kulizungumzia kwa kinagaubaga na nikipata nafasi siku nyingine nitakupa muhtasari wa yale tuliyojadili kwa siku ile kwani nadhani yalikua na mantiki kubwa katika mwenendo was siasa za nchi yetu.Ningetamani sana kama ungekua unatenga mda wa kubadilishana mawaidha na kijana huyo mara kwa mara kwani naamini ni hazina kubwa katika siasa za chama chako na taifa letu kwa ujumla.

Mheshimiwa Rais,nimekua nikikerwa sana na kauli ya "Siasa ni mchezo mchafu" na kama hali hii itaachwa iendelee ni wazi kua hata raia wako wote wanapaswa kuamini kua hata wachezaji wenyewe wa mchezi huo pia ni wachafu!!Sasa mimi sitaki kuamini kua na wewe ni miongoni mwao na kamwe sipaswi niaminishwe hivyo kwani dhamira yako naamini ni safi.Katika hili una jukumu kubwa la kutuonyesha kua sivyo na usikubali hata siku moja watu wasio na ubia na urais wako wakuchafue,tungependa ubaki mweupe kama theluji ili Tanzania uliyotuahidi ionekane.Hakika ukiamua uwezo utatamalaki.

Mheshimiwa Rais, hivi unajua 2010 haiko mbali? Unajua kua siku hiyo utasimama peke yako kuwapigia magoti watanzania wale wale wa 2005? Sasa kwanini ukubali wachezaji wako wakusababishe ushindwe kufika nusu fainali wakati uwezo wa kubadilisha timu ya ushindi unao? Usikubali wananchi wakaja na kauli ya "samaki mmoja akioza….."Hii ni hatari sana mheshimiwa rais mtanzania mwenzangu ambaye ningependa pia uingie katika awamu nyingine ya utawala wa kipindi kingine cha miaka mitano hadi 2015.

Mheshimiwa Rais,Unalo jukumu la kututhibitishia kua utenguzi wa gavana Balali haukufanywa katika misingi ya KUTOLEWA KAFARA.Nakumbuka mwaka 2001 wakati naanza shahada yangu ya kwanza ya siasa na utawala katika chuo kikuu cha Dar Es Salaam,mheshimiwa rais mstaafu wa awamu ya tatu alikuja kuzindua majengo ya hostel za mabibo ambazo kwa kiasi kikubwa zilisaidia kutatua tatizo la malazi kwa wanafunzi.Sisi tulikua watu wa mwanzo kutumia hosteli zile na kila mwanafunzi alikua akisifia mradi ule kwa maneno mafupi sana na yenye kuonyesha imani na viongozi wao.Napenda kuwanukuu "HAKIKA HAYA NI MATUMIZI MAZURI YA FEDHA ZETU".

Mheshimiwa Rais, hivi unajua majengo hayo yaligharimu kiasi gani? Ni shilingi bilioni 16 tu basi.Sasa jaribu kutumia taaluma yako ya MAGAZIJUTO uweze kujua tungekua na majengo kama hayo mangapi kwa fedha alizochota Balali na wenzake ambao bado serikali yako haijaamua kuwaweka bayana il umma wa watanzania wajue japo ni wazi kua itazidi kuwapandisha presha na kuwapa magonjwa ya moyo na kisukari.

Mheshimiwa Rais, ongezeko kubwa la idadi ya wanafunzi katika vyuo vikuu vyetu nchini limezidi kuongeza ukubwa wa tatizo la malazi na sina hakika kama wasaidizi wako katika wizara husika wanakupa uhalisia wa tatizo hili kwani naamini ungeshalitolea tamko kama ilivyo kawaida yako.Siku hizi hosteli za mabibo chumba kimoja wanakaa wanafunzi nane.Hii ni hatari sana kwa afya za vijana wako ambao tunawategemea kama viongozi wetu wa baadae!!!!Tafadhali fanya jitihada turudishiwe hata bilioni 16 katika hizo alizochota balali na wenzake ili tuweze kujenga hostel nyingine kama zile za mabibo ili tupunguze ukubwa wa tatizo hili.

Mheshimiwa Rais,mgongano wa maslahi hasa kwa watumishi wa uma ni kitu hatari sana ambacho kama hakitatafutiwa dawa mapema kinaweza kuiangamiza nchi hii ambayo umedhamiria kuongoza mapambano ya kuikwamua katika umasikini unaoitafuna kwa kipindi kirefu sasa.Tanzania huru bila umaskini inawezekana,TIMIZA WAJIBU WAKO kama ulivyoainisha katika kauli mbiu ya kampeni ya kitaifa ya kupambana na ukimwi.

Mheshimiwa Rais, timu yako ina washambuliaji na viungo hodari sana ambao inakosa ushirikiano kutoka kwa wengine hivyo kushindwa kucheza kama timu.Kuna huyu kiungo wako anaitwa Magufuli, ni hodari kweli kweli ila sehemu ya ukabaji au udhibiti bado butu sana.Hapa nazungumzia hazina ambayo wewe binafsi ulithubutu kuiita roho ya uchumi wa nchi.Kwanini mabadiliko yasianzie hapo mheshimiwa? Au katika hili tutumie ule msemo wa mambo mazuri…na kima ndivyo mheshimiwa rais tutakua hatujachelewa kweli??.Bado tuna imani na wewe na hakika iko siku watumishi wababaishaji watajua wewe ni nani ila tafadhali sana usichelewe kulifanikisha hili mheshimiwa kwani waswahili hao hao waliotoa msemo huo wa mambo mazuri… wanatuonya pia kua ngoja ngoja huumiza matumbo. Wewe ni mtu mzima na makini mheshimiwa rais na unajua hapa namaanisha nini.

Mheshimiwa Rais,kuna suala la EPA(Economic Partnership agreement) au ushirikiano wa kibiashara kati ya nchi zetu za afrika mashariki na jumuia ya ulaya ambalo lilipata kujadiliwa bungeni ila nasikitika kusema kua majibu yaliyotolewa na mshambuliaji wako hayakukidhi haja bali yalijengwa katika misingi ya ushabiki sana kuliko uhalisia wa jambo lenyewe.Hivi ni yapi mema tunayoweza kusema wenzetu wa nchi za Pacific na carebean wamenufaika nayo na sisi tukashawishika kujiunga katika ushirikiano huo? Nisilaumu sana kwani niligundua baadae kua ufahamu wa wabunge wengi hasa wa chama tawala katika hilo ulikua si wa kuridhisha ndo maana ukimya mwingi ulitawala wakati wa mjadala na kuachiwa viongozi wa upinzani kuteka hoja hiyo ambayo baadae ilihitimishwa bila ushawishi wa kimantiki wa nchi yetu kuingia katika huo ushirikiano.

Mheshimiwa Rais, naomba hilo la EPA nilitafutie mda mwingine ili niweze kumalizia kwa kusisitiza machache.Mosi, endelea kutambua kua sisi watanzania tuna imani kubwa kwako ila tumechoshwa na utendaji wa baadhi ya wasaidizi wako.Mbili, watanzania bado wana shauku kubwa ya kupata undani wa kujua yaliyojiri katika ripoti ya Richmond na kwenye ripoti ya Ernst & Young ya ukaguzi wa mahesabu ya akaunti ya madeni ya nje au kwa kitaalamu External Payment Arears Account (EPA).

Mheshimiwa Rais,hivi ile tovuti ya serikali uliyoisimamia kidete iundwe si ndo ingekua mahali muafaka wa kuanika ripoti hiyo ili kuendeleza falsafa ya uwazi iliyosisitizwa na mkuu aliyekutangulia ambaye ni wazi kua hakufanikiwa kuiishi falsafa yake!Ni kweli iliyo wazi kua kama hilo lingefanyika imani kuu na ushirikiano ulio tukuka ungeupata kutoka kwa watanzania wenzako ambao wengine wamefikia hatua ya kuwaita WADANGANYIKA.Hili mimi silikubali hata kidogo mheshimiwa rais na naomba uniunge mkono katika msimamo wangu huo kutokana na ukweli kua sisi watanzania ni watu makini na tukiamua tunaweza kufanya lolote lile.

Mheshimiwa Rais, kwa leo naomba kuwasilisha hayo machache ambayo pengine kwa maoni ya wengine yanaweza kua kero ila kwa mujibu wa katiba yetu uliyoapa kuilinda na kuitetea inatoa fursa hiyo kwa mtu binafsi kama mimi nilivyofanya kuelezea dukuduku langu a mtazamo wangu juu ya nchi yangu ninayoipenda sana ambayo nina ndoto kua siku moja inaweza kua kama PARADISO.

Mheshimiwa Rais, Natamani sana niendelee kuandika kuhusu bodi ya mikopo ya elimu ya juu ila mda nao unanitupa mkono lakini naahidi kutekeleza hili siku za usoni kwani hili ni eneo jingine ambalo USANII usio na mfano umetawala kwa kiwango cha juu sana.Naahidi siku hiyo nitakusimulia kisa cha kweli cha binti mmoja kutoka katika familia ya kimaskini sana ambaye alikosa haki yake ya msingi ya kuendelea na elimu ya juu kutokana na vigezo vya ajabu vilivyowekwa na bodi hiyo ambayo imekua kama wasanii wa kizazi kipya wa kuonekana wenye luninga kila mara pasipo kua na jipya lenye kutia moyo na tumaini kwa wanafunzi wanaohitaji huduma hiyo.Majibu mepesi mepesi yanayotolewa na wenye dhamana katika wizara husika ni ya kukatisha tamaa na sina maneno mbadala zaidi ya kusema ni kama MSIBA mwingine uliyoipata sekta ya elimu ya juu nchini.

Nakutakia afya njema na kazi njema mheshimiwa rais kwani bila wewe hakika chombo hiki (TANZANIA) kitapigwa na mawimbi na hatimaye kitazama bila kuokoa wahanga hata mmoja.Nia na uwezo unao mheshimiwa rais, sasa kwanini usiviruhusu vitamalaki!!!

Ni mimi raia wako mtiifu,

Friday, May 18, 2007

KAULI YA JAJI MKUU SAMATA IWE CHANGAMOTO KWA WADAU WA SHERIA NCHINI



Katika mamabo ambayo watanzania tumekua tukijigamba na kutembea vifua mbele ni AMANI iliyotawala nchini tangu tulipopata uhuru karibu miongo minne na nusu iliyopita..Nchi yetu imetokea kua kimbilio la wageni kutoka nchi majirani ambapo hapakaliki kutokana na kutoelewana na vita vya wenyewe kwa wenyewe na vita vya kimakundi au kimatabaka kati ya watawala na wananchi wao.


Sina haja ya kuingia kwa undani katika hali tete inayoendelea kwa majirani zetu ila kwa kuanzia mada iliyobeba kichwa cha habari hapo juu niliona ni busara kugusua kwa uchache maswahibu yanayowakumba wenzetu katika siasa zao na mifumo ya utawala na ya kutetetea haki zao.


Jana Mheshimiwa jaji mkuu Barnabas Samatta aligusia juu ya umuhimu wa vyombo vya sheria hasa mahakama katika kudumisha amani ya nchi husika kwa kuweka bayana kua...nanukuu "Iwapo jamii itapoteza imani kwa mahakama zetu ndio itakua mwanzo wa kupoteza amani nchini" Inawezekana ikaonekana ni sentensi fupi na iliyozoeleka lakini suala linabaki kua ni jitihada zipi zimefanyika katika kunusuru hali hiyo isitokee???Tunafanya nini ili kuhakikisha wananchi wetu hasa wale waliokata tamaa hawapotezi imani kwa vyombo vyetu hivi ambavyo ni mhimili muhimu katika utawala wa kidemokrasia na wenye kuheshimu haki za binadamu????


Kauli hii imekuja wakati muafaka wakati kukiwa na malalamiko mengi juu ya ubabaishaji unaofanywa na vyombo hivi katika kutetea haki za wanyonge.....Kumekua na ucheleweshaji wa kesi katika kiwango cha kukatisha tamaa na hata mara nyingine kutolewa maamuzi ambayo wakati mwingine yamekua yakizua mjadala juu ya umakini wa vyombo vyetu hivi..Sina nia ya kubeza kila jema linalofanywa na na mahakama zetu ila ni katika kuleta changamoto kwenye mchakato wa wadau kuelekea kwenye ujenzi wa jamii wenye kuheshimu haki za wananchi wenzetu..


Kumekua na migogoro mingi kati ya mtu na mtu,jamii na jamii,wananchi na serikali,wafanyakazi na waajiri wao,wanafunzi na uongozi wao lakini je "nii hatma ya kelele na tofauti zitokanazo na misuguano ya makundi hayo"?? Siku zote binadamu amekua na tabia ya kujaribu njia mbadala pale anapoona nia na mitazamo yao haiendi sawa na kama walivyotaraji....vitendo vya kuchoma vibaka moto ni kielelezo kirahisi cha kuelezea kuchoshwa na ufanisi wa baadhi ya taasisi au asasi zilizokabidhiwa majukumu ya kusimamia mambo kama hayo....Kwanini raia ambaye amechoshwa na tabia ya jambazi sugu au vibaka wazoefu asiamue kuchukua sheria mkononi wakati kila wanapopoleka malalamiko yao kwenye vyombo husika,hakuna maamuzi ambayo yataonekana kukidhi kero za walalamikaji!!!!!!


Kuna kesi nyingi katika sekta ya madini kati ya wachimbaji wadogo wadogo na wamiliki wa makampuni ya kigeni,kuna kesi nyingi kati ya wafanyakazi na waajiri wao ambazo bado mwisho wake haujulikani,wastaafu kila siku wanatanga na njia katika kufuatilia haki zao lakini bila matumaini yoyote katika yale mambo wanayodai ambayo asilimia 90% ni ya msingi!!!!!! Siku za karibuni kumekua na zoezi la bomoa bomoa katika jiji la Dar Es Salaam na asilimia kubwa ya wahanga wa tatizo hilo ni machinga.....vibanda vyao vingi vilipitiwa na sulubu hiyo...Sina nia ya kubeza zoezi hilo kwani mantiki yake iko wazi kabisa 'Kupendezesha mandhari ya jiji' hili ni jambo jema na linapaswa kupongezwa na kila mtu lakini swali la msingi ambalo linastaajabisha kila watu makini ni "Kwanini baadhi ya vibanda viachwe" Katika gazeti tando la michuzi alipiga picha ya moja ya vibanda hivyo na kuhoji uhalali wa kuwepo kwake????Watu wengi walichangia na kusema pengine ni cha mkubwa flani!!!je wakubwa hawapaswi kuguswa na sheria????je hao ndo wanapaswa kua juu ya sheria????


Iko mifano mingi ambayo inatia kichefuchefu katika utekelezaji wa mambo ambayo ni ya manufaa kwa wananchi...Nani hajui kua karibu asilimia 60 ya vituo vya mafuta vilivyopo katika jiji la Dar Es Salaam vipo kinyume na sheria???Je wasimamizi wa sheria hizo wako wapi??? au tunataka wananchi waanze kuamini kua hizo ni miradi ya watunga sera na sheria ambao pia wamepewa ruhusa ya kuzivunja???Ni kwanini majibu ya maswali haya yasipatiwe ufumbuzi wa haraka katika kurudisha imani ya wananchi kwa watawala wao?????


Kwa kumalizia napenda kutoa tu changamoto kwa serikali yetu kua makini katika kusimamia na kutatua kero za wananchi wake ili waendelee kua tayari katika kushiriki kikamilifu utekelezaji wa mipango ya maendeleo yao....Naamini kubwa na serikali ya mheshimiwa baba JK kwahiyo chondechonde watendaji msimwangushe katika nia yake njema ya kujenga nchi moja inayoheshimu haki na yenye kuweka mazingira ya kila mmoja kufaidi matunda ya uhuru...Ubabe wa baadhi ya watendaji hayana nafasi kwasasa kwani mwisho wake hautupi matumaini yoyote mazuri.....Mfano mzuri tunao kwa migomo inayoendelea kwa wanafunzi wa elimu ya juu....hii kwangu ni ishara ya kuchoshwa na ubabaishaji wa baadhi ya watendaji.....Nadhani itabidi tuanze kujadili nia ya mtu kama Proffessor msola katika kutumikia wananchi wa jamuhuri yetu hii.....Inatia hasira pale unaposikia WAZIRI flani msomi anawakatia simu wananchi wake eti kwasababu amechoshwa na kero zao!!!!!!!Hili naomba niliongelee siku nyingine...


Naomba kuwasilisha..